Na Mahmoud Zubeiry
|
HALI
ilikuwa tete mwaka 2001, baada ya Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kujitoa
kudhamini Ligi Kuu ya Tanzania Bara ghafla. Bingwa wa mwaka 2001, Simba SC
alitoka mikono mitupu, baada ya TBL waliokuwa wakiidhamini ligi hiyo kupitia
bia ya Safari Lager ‘kuimwaga’.
Kisa
nini? Kapuya huyo! Aliyekuwa Waziri wa iliyokuwa Wizara ya Kazi, Maendeleo ya
Vijana na Michezo, Profesa Juma Athumani Kapuya, ‘aliwaboa’ wadhamini hao kwa
kujiamulia tu kuongeza timu katika Ligi Kuu, kinyume na makubaliano yao na
Chama cha Soka Tanzania (FAT), sasa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
TBL
wakaona ligi haina kanuni, utaratibu wala kuheshimu vipengele vya mikataba ya
udhamini, wakaitema. Wengi miongoni mwa wapenzi wa soka Tanzania waliingiwa
hofu juu ya mustakabali wa ligi hiyo, kwani walijua itarudi kwenye enzi zile za
kucheza kwa ajili ya mapato ya milangoni tu.
Udhamini
unaongeza ladha ya ligi kwa sababu timu zinawania zawadi, mbali na kombe,
zinapata vifaa vya michezo kutoka wadhamini sambamba na kiasi cha fedha za
gharama kama za usafiri na kadhalika, hivyo kujitoa kwa wadhamini- maana yake
ligi ingekuwa chungu kwa klabu.
Akaibuka
mkombozi, kampuni iliyokuwa mpya kabisa ya huduma za simu za mikononi Tanzania,
Vodacom Tanzania na kuingia mkataba wa udhamini wa ligi hiyo na FAT, kuanzia
msimu wa 2002.
Yanga
ya Dar es Salaam ilikuwa klabu ya kwanza nchini kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu
chini ya udhamini wa Vodacom na leo ni miaka 10 tangu ‘Voda’ waanze
kuipendezesha ligi hiyo, kila msimu wakiboresha mambo fulani fulani muhimu.
Mkataba
wa awali ulimalizika mwishoni mwa msimu na tayari makubalino ya mkataba mpya,
kampuni hiyo kuendelea kuibeba ligi hiyo yamefikiwa na utasaniwa wakati wowote
kabla ya kuanza kwa ligi hiyo, Septemba 15, mwaka huu.
Huu
ni msimu wa 49 wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania, ambayo historia yake inaanzia mwaka
1965, wakati aliyekuwa kocha wa timu ya taifa ya Tanganyika kutoka Yugoslavia,
Milan Celebic, aliposhauri kuwapo kwa michuano ya kusaka klabu bingwa ya taifa,
ili kujenga mazingira ya kupata wachezaji wazuri zaidi wa timu ya taifa.
Alisema
kama kutakuwa na ligi, ina maana wachezaji watakuwa wamepata mazoezi ya muda
mrefu katika kujiandaa na ligi, hivyo kuwa rahisi kwake kama mwalimu wa taifa
wakati huo kuona wachezaji walio fiti na kuwachukua kwenye timu ya taifa.
FAT
ilikubali ushauri huo na kuanzisha Klabu bingwa ya taifa, ambayo ilifanyika kwa
mara ya kwanza mwaka 1965, ikishirikisha timu sita tu zilizoteuliwa ambazo ni
TPC ya Moshi, Sunderland (sasa Simba SC), Yanga na Tumbaku ya Kurasini, Dar es
Salaam, Coastal Union na Manchester United, zote za Tanga.
Michuano
hiyo ya kwanza ilifanyika katika viwanja vya Ilala (sasa Karume) na Manispaa wa
Tanga, sasa Mkwakwani na tatizo kubwa lililojitokeza na viongozi wa klabu,
wachezaji na hata viongozi wa FAT, ni kutozielewa vyema kanuni na sheria za
mchezo, hata ikasababisha Yanga wakajitoa na ubingwa ukatolewa kwa Sunderland
(Simba) walioweka historia ya kuwa mabingwa wa kwanza nchini.
Lakini
awali ya hapo, historia inasema kwamba ligi ilikuwa inachezwa Dar es Salaam
pekee tangu mwaka 1929,
ikishirikisha timu za Cosmopolitan, Battalion King's African Rifles (KAR),
Gymkhana Club, Tanganyika Territorial Police, Tanganyika Railways, Government
School na Government Services.
Sunderland
ilifanikiwa kutetea ubingwa wake msimu uliofuata, kabla ya kuutema kwa
Cosmopolitan ya Dar es Salaam
pia mwaka 1967.
Lakini
wakati wote huo, bado Tanzania
ilikuwa haijawa mwanachama wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), hivyo Sunderland hawakuwahi kucheza michuano ya Afrika. Cosmo
ingekuwa ya kwanza kucheza Klabu Bingwa Afrika mwaka 1968 kama isingejitoa,
lakini kwa kujitoa kwao, Yanga ilifungua historia ya ushiriki wa klabu za
Tanzania kwenye michuano ya Afrika mwaka 1969, baada ya kutwaa ubingwa wa Bara
kwa mara ya kwanza mwaka 1968, kabla ya kuutetea mara tatu mfululizo, katika
miaka ya 1969, 1970, 1971 na 1972. Baada ya hapo, Sunderland ikiwa tayari
imebadili jina na kuitwa Simba kurejesha taji lake mwaka 1973.
Simba
ilishindwa kuutetea ubingwa wake msimu uliofuata, 1974 baada ya kupokonywa na
Yanga katika fainali ya kihistoria iliyofanyika Uwanja wa Nyamagana, mjini
Mwanza kwa kuchapwa mabao 2-1.
Mwaka
1975 Yanga iliutema ubingwa huo kwa Mseto
SC ya Morogoro, ambayo
ilipokonywa na Simba msimu uliofuata.
Simba
iliutetea ubingwa huo kwa miaka mitano mfululizo, kuanzia mwaka 1976 hadi 1980.
Siri
ya kutawala kwa Simba kwenye ligi hiyo kwa miaka yote hiyo ni kuyumba kwa Yanga
baada ya kukumbwa na mgogoro mkubwa 1976, uliosababisha kukimbiwa na wachezaji
wote nyota, hivyo kuanza upya kabisa kuunda timu.
Ni
ndani ya kipindi hicho Simba iliweza kulipa kisasi cha kuchapwa mabao 5-0 na
Yanga mwaka 1968, wakati nayo ilipowatandika watani wao hao wa jadi 6-0 mwaka
1977.
Juni
1, mwaka 1968, Yanga iliigaragaza Simba 5-0, mabao yake yakitiwa kimiani na
Maulid Dilunga (sasa marehemu) katika dakika za 18 kwa njia ya penalti na 43,
wakati mengine yalitiwa kimiani na Salehe Zimbwe dakika ya 54 na 89, kabla ya
Kitwana Manara kupachika la kuhitimisha karamu ya mabao dakika ya 86.
Julai
19, mwaka 1977, Simba nayo ililipa kisasi kwa kuibugiza Yanga mabao 6-0,
wafungaji wakiwa ni Abdallah 'King' Kibadeni aliyetikisa nyavu mara tatu katika
dakika za 10, 42 na 89, wakati mengine yalifungwa na Jumanne Hassan 'Masimenti'
dakika za 60 na 73 na Selemani Sanga wa Yanga alijifunga dakika ya 20.
Kufika
mwaka 1981, tayari Yanga ilikuwa imara tena na kufanikiwa kutwaa ubingwa wa
Tanzania Bara, ingawa msimu uliofuata iliutema kwa Pan African.
Kuanzia
mwaka 1982, mfumo wa Ligi ya Tanzania
ulibadilishwa na kukawa na ligi tatu, kwanza ni igi Daraja la Kwanza Tanzania
Bara, Ligi Daraja la Kwanza visiwani Zanzibar
na Ligi Kuu ya Muungano.
Yaani
baada ya kupatikana washindi wawili wa juu wa kila ligi, Bara na Visiwani,
walikutana kwenye Ligi Kuu ya Muungano, kutafuta bingwa wa Tanzania na washindi wake.
Wakati
huo, bingwa wa Ligi ya Muungano alikwenda kucheza Klabu Bingwa Afrika na
mshindi wa pili alicheza Kombe la Washindi.
Baadaye
timu ziliongezwa na kuwa tatu kila upande katika Ligi ya Muungano.
Mwaka
1983, Yanga ilirejesha taji hilo
kwenye himaya yake, ingawa msimu uliofuata ililitema tena kwa Simba. Kwa ujumla muongo mzima wa 1980, taji la
ubingwa wa Ligi Kuu ya Bara lilikuwa la kupokonyana, kwani Simba nayo mwaka
1985 ilipokonywa taji hilo na Yanga, ambayo nayo ililitema kwa timu mpya katika
Ligi Kuu msimu wa 1986, Tukuyu Stars ya Mbeya.
Tukuyu
nayo iliwarejeshea Yanga taji lao mwaka 1987, wakati mwaka 1988 Wagosi wa Kaya,
Coastal Union ya Tanga ilijiingiza katika orodha ya timu zilizowahi kutwaa taji
hilo . Mwaka
1989, Yanga ilifunga orodha ya mabingwa wa muongo huo kwa kutwaa tena ubingwa
wa Bara.
Simba
iliibuka mwaka 1990 na kutwaa ubingwa huo, ikitoka kuponea chupuchupu kushuka
daraja msimu uliopita.
Kupokonyana
taji kuliendelea hata kwenye muongo wa 1990, kwani Simba iliutema ubingwa huo
kwa Yanga mwaka 1991.
Yanga
iliutetea ubingwa huo mara mbili mfululizo katika miaka ya 1992 na 1993, kabla
ya kupokonywa na Simba mwaka 1994. Simba ilifanikiwa kuutetea mara moja 1995.
Mwaka
1996 ndipo Ligi Kuu ya Tanzania Bara ilipozaliwa rasmi chini ya udhamini wa Bia
ya Safari Lager, bia inayozalishwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) na
ikijulikana kama Safari Lager Premier League,
Yanga ndiyo iliyokuwa bingwa wake wa kwanza. Yanga iliutetea ubingwa huo kwa
miaka miwili mfululizo 1997 na 1998. Mwaka 1999, Yanga ikiwa tayari imetwaa
ubingwa kwa matokeo ya uwanjani, aliyekuwa Waziri wa iliyokuwa Wizara ya Kazi
Maendeleo ya Vijana na Michezo, Profesa Juma Athumani Kapuya, alitengua matokeo
hayo kwa kuiongezea Mtibwa Sugar pointi za mezani, hivyo kuipiku Yanga.
Hatimaye Mtibwa ilipata ubingwa wa mezani.
Mtibwa
ilifanikiwa kutetea ubingwa mwaka 2000, kabla ya kupokonywa na Simba msimu
uliofuata, ingawa Yanga iliibuka mwaka 2002 na kuutwaa tena ubingwa huo.
Mwaka
2003 Simba iliyokuwa kali zaidi ilifanikiwa kuutwaa tena ubingwa huo na
kuutetea mwaka 2004 kabla ya kupokonywa na Yanga
2006. Mwaka 2007, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) lilifanya mabadiliko ya
kalenda yake, ikitaka Ligi yake iendane na ligi za Ulaya, hivyo ikaamua kuchezesha
ligi ndogo ya mpito kumpata bingwa na mwakilishi wa Kombe la Shirikisho, kabla
ya Ligi Kuu kuanza rasmi Agosti.
Simba
iliibuka bingwa wa ligi hiyo, baada ya kuifunga Yanga kwenye fainali kwa
mikwaju ya penalti 5-4, kufuatia sare ya 1-1.
Lakini
msimu uliofuata ikiwa chini ya Profesa wa Kiserbia, Dusan Savo Kondic, Yanga
ilifanikiwa kuurejesha ubingwa wake msimu wa 2008 na kutetea ubingwa hata kabla
ya kucheza mechi zake tano za mwisho.
Simba
iliweka rekodi nzuri katika kumbukumbu zake, baada ya kufanikiwa kumaliza ligi
na kuchukua ubingwa bila kufungwa hata mechi moja.
Msimu
uliopita, Simba walianza vizuri na kukaa kileleni kwa kipindi kirefu, lakini
mechi mbili za mwisho iliporomoka na Yanga ikatwaa ubingwa katika siku ya
kufunga pazia la ligi.
Msimu
uliopita, Simba wakiwa chini ya Profesa wa Kiserbia, Milovan Cirkovick walitwaa
ubingwa huo kwa kishindo, wakiwafunga wapinzani wao wa jadi, Yanga mabao 5-0
katika mechi ya marudiano.
Yanga
walisingizia uongozi dhaifu chini ya Mwenyekiti, Wakili Lloyd Baharagu Nchunga
ulisababisha majanga msimu uliopita, lakini sasa wakiwa na uongozi wa nguvu,
chini ya Mwenyekiti, Milionea Yussuf Mehboob Manji, Makamu Mwenyekiti, Clement
Sanga, ambaye yuko njema pia, na Wajumbe ‘vibopa’ pia, akina Abdallah Bin Kleb,
Mussa Katabaro na wengineo wamepania kulipa kisasa.
Ligi
itakuwa tamu. Ligi itakuwa tamu kwa sababu Azam FC, mali ya Said Salim Bakhresa
imejipanga sawa sawa, baada ya kushika nafasi ya pili msimu uliopita, msimu huu
inataka ubingwa.
Unaweza
kusema Ligi Kuu Bara msimu huu itakuwa mbio za farasi watatu, lakini utarajiwe
upinzani pia kutoka kwa Coastal Union, Mtibwa Sugar, Toto African, Kagera
Sugar, Prisons, Polisi Moro, Mgambo Shooting, African Lyon, JKT Oljoro, Ruvu
Shooting na JKT Ruvu, kwani nazo zimejiandaa kikamilifu kubadilisha historia.
Ukweli
ni kwamba pamoja na ligi za jirani zetu Kenya na Uganda kurushwa na Televisheni
ya kimataifa, SuperSport, lakini VPL ni ligi bora kuliko zote hizo na ndiyo
maana nyota wengi wa kigeni wanavutiwa na ligi yetu yenye wachezaji hadi kutoka
Magharibi na Kusini mwa Afrika.
Dosari
chache na ndogo, kama miundombinu mibovu na ufukara wa baadhi ya klabu, ni
changamoto zinazoekelea kuzoeleleka, lakini ipo haja ya kupamabana nazo.
Changamoto
ambazo si vema kabisa tukazizoea ni rushwa katika katika ligi yetu, marefa
wanahongwa na wachezaji wanahongwa- hili katika msimu huu mpya tupambane nalo.
TFF
iboreshe maslahi ya marefa na iwape kwa wakati, ili kukwepa kuwafanya wawe
wanalipwa na klabu- kwa kufanya hivyo, kwa kiasi kikubwa itapunguza marefa
kuhongwa.
Lakini
mtu anapangiwa mchezo Mbeya, anaambiwa aende bila kupewa posho wala nauli-
unategemea akipewa fedha ya klabu kwa masharti ya kupendelea ataikataa huyo?
Hili
lingine la wachezaji kuhongwa, lazima TFF iliundie kitengo cha kuchunguza na
iwe tayari kuchukua hatua, vinginevyo ligi yetu itabakia kuwa ya hivi hivi,
ikiwa inaingia katika msimu wa 49, yaani kama ni binadamu, anaelekea uzeeni
sasa, amekwishauaga ujana huyo.
ORODHA YA MABINGWA
LIGI KUU:
1965:
Sunderland (Dar es Salaam )
1966:
Sunderland (Dar es Salaam )
1967:
Cosmopolitans (Dar es Salaam )
1968:
Yanga
1969:
Yanga
1970:
Yanga
1971:
Yanga
1972:
Yanga
1973:
Simba
1974:
Yanga
1975:
Mseto SC
(Morogoro)
1976:
Simba
1977:
Simba
1978:
Simba
1979:
Simba
1980:
Simba
1981:
Yanga
1982:
Pan African (Dar es Salaam )
1983:
Yanga
1984:
Simba
1985:
Yanga
1986:
Tukuyu Stars (Mbeya)
1987:
Yanga
1988:
Coastal Union (Tanga)
1989:
Yanga
1990:
Simba
1991:
Yanga
1992:
Yanga
1993:
Yanga
1994:
Simba
1995:
Simba
1996:
Yanga
1997:
Yanga
1998:
Yanga
1999:
Mtibwa Sugar (Morogoro)
2000:
Mtibwa Sugar (Morogoro)
2001:
Simba
2002:
Yanga
2003:
Simba
2004:
Simba
2005:
Yanga
2006:
Yanga
2007:
Simba (Ligi Ndogo)
2008:
Yanga
2009: Yanga
2010: Simba
2011: Yanga
2012: Simba SC
2013 ??????
0 comments:
Post a Comment