• HABARI MPYA

    Tuesday, September 11, 2018

    YANGA SC KUENDELEA KUMKOSA MAHADHI LAKINI ‘NINJA’, ABDUL, YONDAN NA KAMUSOKO WAMEREJEA

    Na Lulu Ringo, DAR ES SALAAM
    KLABU ya Yanga SC itaendelea kumkosa kiungo wake, Juma Mahadhi baada ya kuumia katika mchezo Agosti 19 mwaka huu kwenye mchezo wa Kundi D Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya USM Alger ya Algeria. 
    Mahadhi aliingia kipindi cha pili kwenda kuchukua nafasi ya kiungo Pius Buswita, lakini hakumaliza mchezo baada ya kuumia naye akampisha Ibrahim Ajib.
    Maumivu hayo yameendelea kumuweka nje na leo Mratibu wa Yanga, Hafidh Saleh amesema kwamba mchezaji huyo amepewa mapumziko ya kujiugiza zaidi. 
    Hafidh amesema kwamba majeruhi wengine waliokosekana kwenye mechi ya kirafiki dhidi ya African Lyon Jumapili Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam Yanga ikishinda 1-0, mabeki Juma Abdul, Abdallah Shaibu ‘Ninja’ na Kelvin Yondani na kiungo Thabani Kamusoko wamepona. 
    Juma Mahadhi (kushoto) ataendelea kukosekana Yanga SC baada ya kuumia Agosti 19, mwaka huu

    Hafidh amesema kwamba watatu hao wamejiunga na wachezaji wenzao mazoezini, Uwanja wa Chuo cha Maofisa wa Jeshi la Polisi, Kurasini Dar es Salaam  kujiandaa na mchezo ujao wa Ligi Kuu dhidi ya Stand United Jumapili Uwanja wa Taifa pia.
    “Wachezaji wanaendelea vizuri Ninja alikuwa ana tatizo la bega anaendelea vizuri, Kamusoko yeye alikuwa anasumbuliwa na nyama za paja leo amefanya mazoezi ya kucheza pasi fupi, Yondani aliumia akiwa na timu ya taifa ndiyo maana hakucheza kule Uganda, lakini sasa yuko vizuri, Mahadhi amepewa mapumziko ya muda mfupi ili auguze majeraha aliyonayo,”amesema Hafidh.
    Tofauti na timu nyingine zimecheza mechi mbili hadi tatu, Yanga imecheza mechi moja tu katika Ligi Kuu dhidi ya Mtibwa Sugar na kushinda 2-1, mabao yake yakifungwa na Kelvin Yondani na Heritier Makambo la wapinzani likifungwa na Haroun Chanongo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC KUENDELEA KUMKOSA MAHADHI LAKINI ‘NINJA’, ABDUL, YONDAN NA KAMUSOKO WAMEREJEA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top