• HABARI MPYA

    Saturday, September 22, 2018

    KASEJA ASEMA YANGA ILIWASAIDIA KUWAPIGA STAND UNITED KIULAINI JANA, ATABIRI KMC ITATISHA BAADAYE WATU HAWATAAMINI

    Na Lulu Ringo, DAR ES SALAAM
    NAHODHA wa KMC, Juma Kaseja amesema kwamba walifanikiwa kuwafunga kwa urahisi Stand United jana kwa sababu walikuwa wana uchovu baada ya kutumia nguvu nyingi kwenye mechi dhidi ya Yanga SC.
    Stand United ilichapwa 2-0 jana Uwanja wa Uhuru na KMC iliyopanda Ligi Kuu msimu huu, ikitoka kuchapwa 4-3 na Yanga SC Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam katika mchezo uliotangulia.
    Na akizungumza na Waandishi wa Habari baada ya mchezo wa jana, Kaseja alisema kwamba walicheza kwa kushambulia kwa sababu walijua wapinzani wao watachoka kwa kuwa wametoka kucheza mechi kubwa dhidi ya Yanga.

    Juma Kaseja amesema waliifunga kwa urahisi Stand United jana kwa sababu walikuwa wana wa mechi na Yanga SC

    “Tunamshukuru Mungu tumepata ushindi wa kwanza, lakini ukiangalia hata mechi tuliyopoteza juzi na Singida tulitengeneza nafasi nyingi tukakosa. Leo mwalimu alituambia tupeleke mbele na tushambulie kwa sababu wametoka kucheza mchezo mkubwa na Yanga watakuwa wametumia nguvu nyingi sana, kwa hiyo kuna kipindi watakata,”alisema kipa huyo wa kwanza wa zamani wa taifa.
    Kaseja alisema kwamba kwa kufuata maelekezo ya kocha wao, Mrundi Ettienne Ndayiragijje walishambulia kwa nguvu kipindi cha kwanza na wanashukuru Mungu walifanikiwa kupata magoli mawili.
    Kuhusu wachezaji chipukizi wengi kikosini KMC, Kaseja amesema kwamba kuna changamoto nyingi na kikubwa ni kuingiwa na hofu kwenhye baadhi ya mechi, kwa sababu wametokea Ligi Daraja la Kwanza na sasa wapo Ligi Kuu.
    “Lakini ukiangalia kadiri tunavyozidi kucheza na wao wanazidi kuzoea, kwa hiyo mimi naamini huko mbele timu itafanya kitu kizuri ambacho kitakuja kuwashangaza watu wengi,” amesema kipa huyo wa zamani wa klabu zote, Simba na Yanga.
    Kwa upande wake, kiungo wa KMC Abdallah Masoud ‘Cabaye’ anayecheza kwa mkopo kutoka Azam FC amesema kwamba ushindi wa jana umewapa taswira mpya ya kufanya vizuri.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KASEJA ASEMA YANGA ILIWASAIDIA KUWAPIGA STAND UNITED KIULAINI JANA, ATABIRI KMC ITATISHA BAADAYE WATU HAWATAAMINI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top