NYOTA wa Simba SC, kiungo Msenegal Alassane Maodo Kanté na mshambuliaji Mghana, Jonathan Sowah wamefungiwa mechi tano kila mmoja na kutozwa Faini ya Sh. Milioni 1 kila mchezaji kwa makosa ya kinidhamu kwenye mechi ya Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara dhidi ya Azam FC Desemba 7 Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Wakati Kante amepewa adhabu hiyo kwa kumpiga teke kwa makusudi kiungo wa Azam FC, Feisal Salum Abdallah – Sowah ameadhibiwa kwa kosa la kumpiga kiwiko kiungo mwingine wa Azam FC, Himid Mao Mkami katika mchezo ambao Azam FC iliibuka na ushindi wa 2-0, mabao ya mshambuliaji Mkongo, Jephte kitambala Bola dakika ya 81 na winga Iddi Suleiman Nado dakika ya 89.
Wawili hao wameadhibiwa baada ya kukutwa na Hatia katika kikao cha Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) cha kupitia mwenendo na matukio mbalimbali ya Ligi Kuu siku za karibuni kilichofanyika Desemba 15 Jijini Dar es Salaam.
Aidha, kikao hicho pia kimemuondoa refa wa mchezo huo Abdallah Mwinyimkuu kwenye orodha ya waamuzi wa Ligi Kuu kwa mizunguko mitano kwa kushindwa kuchukua sahihi dhidi ya wachezaji hao mara tu walipoyatenda.
Katika kikao hicho cha Bodi, kiungo Mganda wa Singinda Black Stars, Khalid Aucho amefungiwa mechi tano pia na kutozwa faini ya Sh. Milioni 1 kwa kosa la kumsukuma mchezaji wa TRA United, Adam Adam, huku refa wa mchezo huo, Alex Pancras akipewa onyo kali kwa kosa hilo.





.png)
0 comments:
Post a Comment