• HABARI MPYA

    Sunday, September 30, 2018

    KOCHA MSAIDIZI AZAM FC, JUMA MWAMBUSI AWATAKA MAREFA KUTENDA HAKI LIGI KUU

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KOCHA Msaidizi wa Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati Azam FC, Juma Mwambusi, ameweka wazi kuwa timu yake ilistahili kupewa penalti kama waamuzi wa mchezo wao dhidi ya Lipuli wangekuwa watenda haki.
    Mchezo huo wa Ligi Kuu Tanzania Bara (TPL) uliofanyika Uwanja wa Azam Complex jana Ijumaa usiku ulimalizika kwa suluhu matokeo yaliyoifanya Azam FC kusalia nafasi ya nne kwenye msimamo wa ligi ikiwa na pointi 12.
    Kuelekea dakika 15 za mwisho za mchezo huo, mwamuzi Meshack Suda kutoka Singida na Msaidizi wake namba moja, Jesse Erasmo (Morogoro) walipeta kwa kushindwa kuipa penalti Azam FC baada ya mshambuliaji Donald Ngoma, kuguswa na mikono na kipa wa Lipuli wakati akiwa kwenye harakati za kufunga bao.
    Akizungumza mjini Dar es Salaam mara baada ya mchezo huo, Mwambusi alisema waamuzi bado hawajawa makini sana kwenye asilimia kubwa ya mechi walizocheza huku akidai kila mtu anayefanya vizuri inatakiwa apate haki yake.
    Juma Mwambusi (kulia) ameomba marefa watende haki katika uchezeshaji wao

    “Kikubwa tunashukuru mpira umeisha bila majeraha kwa wachezaji ni masikitiko yetu tulikuwa tunataka kupata pointi tatu na tumeondoka na pointi moja hilo ni masikitiko kwa sababu hatukutarajia, lakini binadamu anatakiwa awe katika haki ya kutenda haki hususani waamuzi katika mchezo.
    “Unajua hata penalti ukishinda ukipata goli inamaana pointi tatu unapata kwa hiyo tumepata penalti mwamuzi hakuweza kutupa kwa hiyo tumesumbuka na ligi hii tukikutana na waamuzi bado hawajakuwa makini sana katika kuhakikisha wanatenda haki katika mchezo kila mtu anayefanya vizuri basi lazima apate haki yake,” alisema.
    Alisema kwa sasa wanajipanga kwa ajili ya mchezo ujao dhidi ya Tanzania Prisons utakaofanyika Jumanne ijayo kwenye Uwanja wa Azam Complex akidai wanatakiwa kuhakikisha wanafanya vizuri.
    “Wachezaji wanalijua hilo tuna jukumu letu kushinda hatuwezi kusogea kwenye msimamo wa ligi bila kupata pointi tatu kwa hiyo nadhani hii imeisha (Lipuli) tunaisahau na tunangoja inayokuja (Tanzania Prisons),” alisema.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KOCHA MSAIDIZI AZAM FC, JUMA MWAMBUSI AWATAKA MAREFA KUTENDA HAKI LIGI KUU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top