TIMU ya Mamelodi Sundowns FC imeingia Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya kuwatoa mabingwa watetezi, Al Ahly kufuatia sare ya 1-1 leo Uwanja wa Cairo International Jijini Cairo nchini Misri.
Mamelodi Sundowns wanakwenda Fainali kwa faida ya mabao ya ugenini kufuatia sare ya bila mabao katika mchezo wa kwanza Aprili 19 Uwanja wa Loftus Versfeld Jijini Pretoria, Afrika Kusini.
Katika mchezo wa marudiniano leo, mshambuliaji Taher Mohamed alianza kuwafungia Ahly dakika ya 24, kabla ya Yasser Ibrahim kujifunga dakika ya 90 kuitemesha tonge kinywani timu yake na kuipeleka Fainali Mamelodi.
Matokeo haya yanamaanisha Ahly inavuliwa taji hilo baada ya kukaa nalo kwa misimu miwili mfululizo, wakati Mamelodi wanakwenda Fainali kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2016 walipotwaa taji hilo kwa ushindi wa 3-0 nyumbani na kipigo cha 1-0 ugenini.
Mamelodi Sundowns sasa wanasubiri mshindi kati ya Pyramids ya Misri na Orlando Pirates ya Afrika Kusini kukutana naye katika Fainali - timu ambazo zinarudiana muda huu Uwanja wa Jeshi la Anga wa Juni 30 Jijini Cairo.
0 comments:
Post a Comment