• HABARI MPYA

    Saturday, May 24, 2014

    TAIFA STARS, MALAWI KUPAMBANA JUMANNE

    Na Boniface Wambura, DAR ES SALAAM
    TIMU ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars itacheza na Malawi, Flames Jumanne (Mei 27 mwaka huu) katika mchezo wa kirafiki utakaofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 11:00 jioni.
    Mechi hiyo itakuwa ya mwisho kwa Taifa Stars kujipima kabla ya kucheza mchezo wa marudiano wa michuano ya Afrika na Zimbabwe (Mighty Warriors) utakaofanyika Juni Mosi mwaka huu jijini Harare.
    Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager ipo kambini Tukuyu mkoani Mbeya chini ya Kocha wake Mart Nooij kujiandaa kwa mechi dhidi ya Malawi na ile ya Zimbabwe.
    Taifa Stars iliyoilaza 1-0 Zimbabwe Jumanne itakuwa na kazi na Malawi Taifa 

    Malawi imewasili leo mchana (Mei 24 mwaka huu) kwa ndege ya Malawian Airlines kwa ajili ya mchezo huo ikiwa na msafara wa watu 27, na imefikia kwenye hoteli ya Sapphire Court iliyopo Mtaa wa Lindi jijini Dar es Salaam.
    Flames inayofundishwa na mchezaji wa zamani wa kimataifa wa Malawi, Young Chidmozi inatarajia kufanya mazoezi leo jioni Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume.
    Baada ya mechi hiyo, Malawi itakwenda moja kwa moja nchini Chad kwa ajili ya mechi ya marudiano ya michuano ya Afrika itakayochezwa Mei 30 mwaka huu jijini Ndjamena.
    Taifa Stars iliifunga bao 1-0 Zimbabwe katika mchezo wa kwanza wa mchujo kuwania kupangwa kwenye makundi ya kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Mataifa ya Afrika 2005 nchini Morocco, uliofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam Jumapili iliyopita.
    Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Joseph Odartei Lamptey aliyesaidiwa na Malid Alidu Salifu na David Laryea wote wa Ghana, hadi mapumziko Taifa Stars walikuwa mbele kwa bao hilo 1-0.
    Bao hilo lilifungwa na mshambuliaji wa Azam FC, John Bocco ‘Adebayor’ dakika ya 13 akiunganisha kwa guu la kushoto krosi maridadi ya mshambuliaji wa TP Mazembe ya DRC, Thomas Ulimwwengu.
    Nayo Malawi, iliichapa Chad mabao 2-0 Ijumaa ya wiki iliyopita katika mechi nyingine ya michuano hiyo, mabao ya Frank ‘Gabadinho’ Uwanja wa Kamuzu mjini Blantyre.
    Mshambuliaji huyo wa Bloemfontein Celtic, ambaye anatarajiwa kushinda tuzo ya Mchezaji Bora Chipukizi wa Mwaka wa Ligi Kuu ya Afrika Kusini (PSL), aliifungia The Flames bao la kwanza dakika ya tano.
    Alifunga bao hilo akimtungua kipa wa Chad Dillah Mbiramadji kumalizia mpira wa adhabu uliopigwa na Joseph Kamwendo. Alifunga bao la pili dakika ya 73 baada ya kuwazidi mbio mabeki wa Chad katika kuukimbilia mpira mrefu, ambao alipoufikia alikimbia nao kabla ya kufunga.
    Malawi na Tanzania zitasafiri kuwafuata Chad na Zambia baada ya mchezo wa Jumanne na washindi wa jumla baada ya mechi za marudiano wataingia katika hatua ya mwisho ya mchujo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TAIFA STARS, MALAWI KUPAMBANA JUMANNE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top