• HABARI MPYA

    Wednesday, May 28, 2014

    MALINZI AWATAKA VODACOM KUBORESHA ZAWADI LIGI KUU TIMU ZOTE ZINUFAIKE

    Na Renatus Mahima, DAR ES SALAAM 
    RAIS wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi amewataka wadhamini wakuu wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL), kampuni ya huduma za simu ya Vodacom Tanzania kuangalia upya mfumo wa utoaji zawadi ili kila timu inayoshiriki ligi hiyo iambulie kitu.
    Akitoa hotuba yake katika hafla ya kukabidhi zawadi za ligi hiyo msimu huu iliyofanyika kwenye Jengo la Golden Jubilee jijini Dar es Salaam usiku wa kuamkia leo, Malinzi amesema kuna haja ya kuuangalia upya utaratibu wa utoaji zawadi ili kila timu inayoshiriki ligi kuu ipate zawadi.
    Rais wa TFF, Jamal Malinzi akizungumza jana

    "Fomula ya utoaji zawadi lazima ipitiwe upya ili kila timu ipewe zawadi, bingwa apate Sh. milioni 100 (mfano) na timu ambazo hazijapata fursa ya kuingia kwenye nafasi za zawadi nazo zipewe walau kifuta jasho cha Sh. 500,000," amesema Malinzi.
    "Hata timu zinazopanda daraja lazima zipewe fungu kuziwezesha kupambana na timu ambazo zina wachezaji wa gharama kubwa. Wale Ndanda FC, Stand United na Polisi Morogoro zilipaswa kupewa fungu la kuzikaribisha ligi kuu. 
    "QPR imepewa pauni milioni 125 baada ya kupanda tena Ligi Kuu ya England," amesema zaidi Malinzi huku akiweka wazi kwamba wataanza mazungumzo muda si mrefu na Vodacom Tanzania ili waingie mkataba mpya.
    Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Masoko wa kampuni hiyo, Kelvin Twisa, amesema wamefurahishwa na ushindani mkali uliooneshwa na timu zote 14 msimu huu na wataongeza mkataba wa kuendelea kuidhamini ligi hiyo baada ya uliopo kumalizika msimu ujao.
    "Tunawashukuru sana bodi ya ligi kuu (TPLB) kwa kugawa vizuri fungu tunalolitoa kwa timu na vifaa vya marefa. Tunawashukuru pia kampuni ya Azam Media kwa kudhamini ligi hiyo na kuongeza hamasa. Tunaomba waje wadhamini wengine tusaidie kuinua soka la Tanzania," amesema Twisa.
    Silas Mwakibinga, Ofisa Mtendaji Mkuu (CEO) wa TPLB, amesema msimu huu ulikuwa na changamoto nyingi zikiwamo za fujo na uhuni wa mashabiki viwanjani, uhujumu wa mapato kutokana na kutotumika kwa tiketi za elektroniki, maamuzi mabovu ya marefa na migogoro ya timu inayofifisha matokeo na mapato ya mlangoni.
    Mwakibinga amesema jumla ya mashabiki 728,600 waliingia viwanjani kwa kukata tiketi halali ikiwa ni ongezeko ikilinganishwa na msimu uliopita ambao waliingia mashabiki 652,089.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MALINZI AWATAKA VODACOM KUBORESHA ZAWADI LIGI KUU TIMU ZOTE ZINUFAIKE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top