• HABARI MPYA

    Wednesday, May 28, 2014

    POLISI ZENJI YATOLEWA KAPA SUDAN, MBEYA CITY WASAKA ROBO FAINALI LEO

    Na Rodgers Mulindwa,  KHARTOUM
    POLISI ya Zanzibar imefungishwa virago mapema katika michuano ya Nile Basin inayoendelea nchini Sudan, baada ya jana kufungwa mabao 3-0 na Victory University ya Uganda.
    Mabao yaliyowazamisha Maaande wa Jeshi la Polisi visiwani Zanzibar jana yamefungwa na Mutyaba Muzamir dakika ya 39 na Kibirige Jackson dakika ya 45 na 48.
    Huo ni mchezo wa tatu mfululizo Polisi wanafungwa na maana yake wanaiacha michuano hiyo mipya ya Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) baada ya hatua za makundi.

    Awali katika michuano hiyo inayoshirikisha mabingwa wa FA au washindi wa pili wa Ligi Kuu za nchi wanachama wa CECAFA,  Polisi walifungwa na Malakia ya Sudan Kusini na wenyeji El-Merreikh. Matokeo hayo yanaifanya Victoria imalize katika nafasi ya pili, wakati Malakia imemaliza nafasi ya tatu katika Kundi hilo.
    Merreikh imemaliza kileleni mwa Kundi hilo kufuatia ushindi wa mabao 4-2 dhidi ya jirani zao, Malakia. Mabao ya Merreikh yalifungwa na Pascal Wawa dakika ya sita, Kor Traore dakika ya 26, Tia Togbi Olivier dakika ya 42 na Sadjo Haman dakika ya 88, wakati ya Malakia yalifungwa na John William dakika ya 72 na Thomas Jacob dakika ya 80. Merreikh imemaliza na pointi saba sawa na Victoria University, lakini yenyewe inapaa kileleni kwa wastani mzuri wa mabao ya kufunga na kufungwa.
    Wakati huo huo, wawakilishi wengine wa Tanzania, Mbeya City leo wanashuka dimbani kucheza mechi yake ya mwisho ya Kundi B dhidi ya Enticelles ya Rwanda ikihitaji ushindi ili kwenda Robo Fainali.
    Mbeya City ina pointi tatu hadi sasa baada ya kushinda mechi moja na kufungwa moja. AFC Leopard iliyo kileleni mwa Kundi B yenyewe itamaliza na Academie Tchite ya Burundi, ambayo ikishinda itakuwa na nafasi ya kusonga mbele pia.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: POLISI ZENJI YATOLEWA KAPA SUDAN, MBEYA CITY WASAKA ROBO FAINALI LEO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top