• HABARI MPYA

    Monday, May 26, 2014

    MBEYA CITY NA AFC LEOPARD PATACHAFUKA KHARTOUM LEO, POLISI ZENJI NI YA KUJIPIGIA TU SUDAN

    Na Mwandishi Wetu, KHARTOUM
    MBEYA City inashuka dimbani leo kwenye Uwanja wa Khartoum, Sudan kumenyaa na AFC Leopard ya Kenya katika mchezo wa Kundi B michuano mipya ya Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), Nile Basin inayoendelea nchini hapa. 
    Timu hiyo ya Halmashauri ya Jiji la Mbeya leo itahitaji ushindi mwingine baada ya kuifunga Academie Tchite ya Burundi 3-2 katika mchezo wa kwanza ili kujihakikishia kutinga Robo Fainali.
    Kocha wa Mbeya City, Juma Mwambusi akiiongoza timu yake juzi nchini Sudan. Leo ana mtihani mbele ya AFC Leopard ya Kenya

    Timu hiyo ya kocha Juma Mwambusi ilicheza soka ya kuvutia katika mchezo wake wa kwanza juzi licha ya makosa madogo madogo ya safu ya ulinzi na tayari imeingizwa kwenye moja ya timu zinazotarajiwa kufika mbali.
    Ikiwa imeongezewa nguvu na mshambuliaji mpya kutoka Kagera Sugar, Themi Felix Buhaja, Mbeya City sasa ina safu kali ya ushambuliaji ambayo vigumu kulala njaa.
    Themi Felix pamoja na washambuliaji wengine wawili walioibeba timu hiyo kwenye Ligi Kuu msimu uliomalizika, Paul Nonga na Mwagane Yeya ndiyo waliofunga kwenye ushindi wa juzi.
    Mchezo wa Mbeya City na Leopard utaanza Saa 2:00 kwa saa za Sudan, baada ya mchezo kati ya Academie Tchite na Enticelles ya Rwanda.
    Wakati huo huo: Polisi ya Zanzibar jana imepoteza mechi ya pili mfululizo Kundi C, baada ya kufungwa mabao 3-0 na Malakia ya Sudan Kusini.
    El-Merreikh imelazimishwa sare ya bila kufungana na Victoria University ya Uganda, wakati Defence ya Ethiopia imeifunga 2-1 Dkhill ya Djibouti.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MBEYA CITY NA AFC LEOPARD PATACHAFUKA KHARTOUM LEO, POLISI ZENJI NI YA KUJIPIGIA TU SUDAN Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top