• HABARI MPYA

    Tuesday, May 27, 2014

    KIPRE TCHETCHE MCHEZAJI BORA TANZANIA, CASILASS WA MTIBWA NDIYE KIPA BORA

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa Azam FC kutoka Ivory Coast, Kipre Herman Tchetche ameshinda tuzo ya mchezaji bora wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara msimu wa 2013-2014 akiwapiku Anthony Matogolo wa Mbeya City na Lugano Mwangama wa Prisons.
    Kwa ushindi huo, Kipre amezawadiwa kitita cha Sh. Milioni 5.2.
    Aidha, kipa wa Mtibwa Sugar ya Morogoro, Hussein Sharrif ‘Cassilas’ ameshinda tuzo ya mlinda mlango bora wa Ligi Kuu akiwapiku David Burhan wa Mbeya City na Beno Kakolanya wa Prisons.
    Meneja wa Azam FC, Jemadari Said akipokea tuzo ya Kipre Tchetche kutoka kwa Rais wa TFF, Jamal Malinzi kulia usiku huu katika hafla iliyofanyika ukumbi wa Golden Jubilee Tower katikati ya Jiji la Dar es Salaam. Mwingine kulia ni Mkurugenzi wa Masoko wa Vodacom, wadhamini wa Ligi Kuu.

    Juma Mwambusi Mwambusi wa Mbeya City, alishinda tuzo kocha bora, akiwaangusha Charles Boniface Mkwasa wa Yanga SC na Mecky Mexime wa Mtibwa Sugar na kupewa Sh. Milioni 5.2. 
    Refa Israel Mujuni Nkongo wa Dar es Salaam ameibuka mwamuzi bora akilamba Sh. milioni 7.8 baada ya kuwabwaga Isihaka Shirikisho wa Tanga na Jonasia Rukia wa Kagera walioingia kwenye kipengele hicho.  
    Tuzo ya Mfungaji bora wa msimu ilikwenda kwa mshambuliaji wa Simba, Mrundi Amisi Tambwe, aliyefunga mabao 19 na kuzawadiwa Sh. Milioni 5.2.
    Azam FC wakipokea zawadi ya ubingwa
    Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Yanga SC, Salum Rupia akipokea zawadinya ushindi wa pili
    Mweka Hazina wa Azam FC, Karim Mapesa akipokea hundi kutoka kwa Mkurugenzi wa Masoko wa Vodacom, Kevin Tisa
    Wadau wa Azam FC katika picha ya pamoja na viongozi wa TFF na wadhamini, Vodacom

    Tambwe aliwashinda Elias Maguri wa Ruvu Shooting, Kipre Tchetce wa Azam FC wote mabao 13, Mrisho Ngassa na Hamisi Kiiza wote wa Yanga SC ambao wote walifunga mabao 12 kila mmoja. 
    Yanga SC imeibuka timu yenye nidhamu kwa mara nyingine baada ya kutwaa tuzo hiyo pia msimu wa 2012/13 wa Ligi Kuu na kuzawadiwa Sh. Milioni 16 ikizipiku Azam FC na JKT Oljoro.
    Zawadi nyingine zilizotolewa ni pamoja na Sh. milioni 75 iliyokwenda kwa Azam FC waliotwaa ubingwa, Yanga SC Sh. milioni 35, Mbeya City Sh. milioni 26 na Simba SC Sh. 21.
    Hakukuwa na mchezaji hata mmoja kati ya walioshinda tuzo zao kutokana na wachezaji hao kuwa mapumzikoni baada ya kumalizika kwa Ligi Kuu na wote walipokelewa tuzo zao.
    Juma Mwambusi yuko Sudan na timu yake wakishirki michuano ya Nile Basin, naye alipokelewa tuzo yake na Katibu Mkuu wake, Emmanuel Kimbe. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KIPRE TCHETCHE MCHEZAJI BORA TANZANIA, CASILASS WA MTIBWA NDIYE KIPA BORA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top