• HABARI MPYA

    Wednesday, May 28, 2014

    KIUNGO WA TP MAZEMBE AJILETA MWENYEWE SIMBA SC

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    KIUNGO wa Tout Puissant Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Joseph Kamwendo amesema anapenda sana kuchezea Simba SC ya Dar es Salaam na amewafungulia milango wakati wowote wakiwa tayari wamfuata kuzungumza naye.
    Akizungumza na BIN ZUBEIRY jana baada ya mchezo wa timu yake ya taifa, Malawi dhidi ya Tanzania Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Kamwendo alisema anaipenda Simba SC. “Tanzania ninaipenda Simba SC, ninaweza kujiunga nayo wakinihitaji, nawakaribisha sana,”alisema mchezaji huyo hodari.
    Mwekundu wa Msimbazi; Kiungo Joseph Kamwendo amesema anapenda kuchezea Simba SC

    Kamwendo aliichezea Malawi ‘Flames’ jana ikifungwa 1-0 na Tanzania, Taifa Stars katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa, timu hizo zikijiandaa na mechi za marudiano za hatua za awali za mchujo za Kombe la Mataifa ya Afrika.  
    Tanzania baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya Zimbabwe na Malawi ikitoka kuifunga 2-0 Chad, zote zitakuwa ugenini wikiendi hii kujaribu kutafuta nafasi ya kusonga mbele kuwania kupangwa kwenye makundi ya kugombea tiketi ya Fainali za Morocco mwakani.
    Kamwendo aliyezaliwa Oktoba 23, mwaka 1986 mjini Blantyre, Malawi alikuwa mchezaji wa kwanza wa kigeni kushinda tuzo ya Mwanasoka Bora wa Mwaka wa Zimbabwe mwaka 2005, wakati huo akiichezea CAPS United.
    Alijiunga na Mazembe, yenye washambuliaji wawili Watanzania, Mbwana samatta na Thomas Ulimwengu Novemba mwaka 2013, kwa Mkataba wa miaka mitano.
    Awali ya hapo, kuanzia mwaka 2003 hadi 2004 alichezea MTL Wanderers na alipotoka CAPS, alikwenda Nordsjaelland ya Denmark hadi mwaka 2006 aliporejea MTL Wanderers, ambako alicheza hadi 
    2007 alipohamia Orlando Pirates ya Afrika Kusini, ambako alicheza hadi alipochukuliwa Vasco da Gama ya Afrika Kusini kwa mkopo mwaka 2010.
    Mwaka 2011 alirejea MTL Wanderers alipocheza hadi 2013 akaenda Liga Muculmana ya Msumbiji ambako baada ya muda mfupi, akahamia TP Mazembe.
    Tangu mwaka 2003, Kamwendo ameichezea Malawi mechi 68 na kuifungia mabao matano.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KIUNGO WA TP MAZEMBE AJILETA MWENYEWE SIMBA SC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top