KLABU ya Chabab Riadhi Belouizdad, maarufu tu kama CR Belouizdad ya Algeria imemsajili kiungo mshambuliaji Muivory Coast, Jean Charles Ahoua (23) kwa mkataba wa miaka miwili na Nusu kutoka Simba SC.
Taarifa ya CR Belouizdad jioni hii imesema; “Tumemsajili mshambuliaji wa Ivory Coast, Jean Charles Ahoua (umri wa miaka 23), akitokea klabu ya Simba ya Tanzania, kwa mkataba wa miaka miwili na nusu,”.
Kocha Mjerumani Sead Ramović mwenye asili ya Bosnia & Herzegovina alivutiwa na Ahoua wakati anafundisha Yanga ya Tanzania mwaka jana ambao ni wapinzani wa jadi wa Simba na sasa ametimiza ndoto za kufanya kazi na mchezaji huyo.
Ahoua aliwasili Simba SC Julai mwaka 2024 akitokea Stella Club aliyojiunga nayo Julai 2022 baada ya awali kuchezea Séwé Sports na LYS Sassandra zote za kwao, Ivory Coast.
Ahoua alikuwa na msimu mzuri uliopita akiibuka Mfungaji Bora wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara kwa mabao yake 16 huku pia akiiwezesha Simba kufika Fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika.
Alikaribia pia kuipa Simba SC ubingwa wa Ligi Kuu kama si kufungwa 2-0 na Yanga katika mechi ya mwisho ya msimu siku ambayo waliiihutaji sare tu kutwaa taji hilo.



.png)
0 comments:
Post a Comment