• HABARI MPYA

    Thursday, July 07, 2016

    NAHODHA WA MAMELODI NA ZIMBABWE ATUA SIMBA SC…NI BEKI LA KATI METHOD MWANJALI

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    NAHODHA wa zamani wa timu ya taifa ya Zimbabwe, Method Mwanjali yuko nchini kwa ajili ya kusajiliwa Simba SC.
    Nahodha huyo wa Caps United ya Zimbabwe amewasili jana na habari zinasema, kiungo wa Simba, Mzimbabwe pia, Justice Majabvi ndiye amemleta mchezaji huyo.
    Mwanjali alikuwepo Uwanja wa Chuo cha Polisi, Kurasini, Dar es Salaam leo asubuhi wakati wa mazoezi ya Simba SC, lakini hakufanya na inaelezewa ataanza kesho.
    Simba inafanya mazoezi Uwanja wa Chuo cha Polisi Kurasini tangu Jumanne na inatarajiwa kuhamia kambini Morogoro Jumapili. 
    Beki wa kati Mzimbabwe, Method Mwanjali yuko nchini kwa ajili ya kusajiliwa Simba SC

    “Majabvi amependekeza mchezaji wa kusajiliwa Simba na tayari amefika nchini, ataanza majaribio kesho,”kimesema chanzo.
    Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe hakupatikana alipotafutwa kwenye simu yake na habari zinasema amekwenda Marekani kwa mapumziko.
    Mwanjali ambaye hivi karibuni alikuwa anakabiliwa na kesi ya kujeruhi katika ugomvi wa klabu ya usiku, alikuwa Nahodha wa kikosi cha Zimbabwe kilichotwaa Kombe la COSAFA Castle mwaka 2009 wakiwafunga mahasimu, Zambia 3-1 katika fainali Uwanja wa Rufaro.
    Amewahi kucheza kwa mafanikio soka ya kulipwa Afrika Kusini katika klabu za Mamelodi Sundowns na Mpumalanga Black Acess za Ligi Kuu ya ABSA ya nchini humo.
    Na Majabvi anamleta mchezaji huyo wakati yeye mwenyewe kuna uwezekano asiwepo kwenye kikosi cha Simba msimu ujao kutokana na mpango wake wa kwenda kuungana na mkewe Australia. 
    Lakini uongozi wa Simba unaendelea kumshawishi abaki kwa mwaka wa mwisho na ataruhusiwa kuondoka mwishoni mwa msimu. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NAHODHA WA MAMELODI NA ZIMBABWE ATUA SIMBA SC…NI BEKI LA KATI METHOD MWANJALI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top