• HABARI MPYA

    Tuesday, July 26, 2016

    YANGA NI KUFA NA KUPONA LEO GHANA, VINGINEVYO NDIYO BASI TENA!

    Na Mwandishi Wetu, SEKONDI
    YANGA SC inahitaji ushindi wa ugenini leo itakapomenyana na wenyeji, Medeama FC Uwanja wa Essipong Sports mjini Sekondi, Ghana ili kufufua matumaini ya kwenda Fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika.
    Yanga imecheza mechi tatu za awali za Kundi A bila ushindi, ikifungwa 1-0 mara mbili na MO Bejaia nchini Algeria na TP Mazembe na kutoa sare na Medeama 1-1 Dar es Salaam.
    Na baada ya matokeo hayo, Yanga sasa inashika mkia katika kundi hilo, ikiwa na pointi moja tu, chini ya Medeama wenye pointi mbili, MO Bejaia pointi tano na vinara Mazembe wenye pointi saba.
    Wachezaji wa Yanga wakifanya mazoezi jana Uwanja wa Essipong ambao utatumika kwa mechi ya leo
    Wachezaji wa Yanga walionekana kuwa kwenye ari nzuri kuelekea mchezo wa leo 
    Je, watapata ushindi wa kwanza leo licha ya kucheza ugenini?


    Ikiingia katika mchezo wa nne leo, Yanga inahitaji ushindi tu kwanza na baada ya hapo iiombee Mazembe iifunge Bejaia ili kuweka hai matumaini ya Nusu Fainali. 
    Mchezo wa leo wa Yanga Medeama utachezeshwa na marefa wa Morocco, ambao ni Redouane Jiyed, atakayepuliza filimbi akisaidiwa na washika vibendera Mohamed Lahmidi na Hicham Ait Abbou.
    Mazembe itaikaribisha MO Bejaia kesho Uwanja wa Mazembe mjini Lubumbashi ikihitaji ushindi ili kujihakikishia Nusu Fainali. 
    Kimahesabu, hata kama Yanga ikifungwa leo, itakuwa na nafasi ya kwenda Nusu Fainali, iwapo itashinda mechi mbili za mwisho dhidi ya Bejaia na Mazembe, lakini pia ni kuziombea matokeo mabaya Medeama na Bejaia. 
    Ila kwa uhalisia wa ushindani na mwenendo wa kundi A, Yanga inahitaji ushindi leo kufufua matumaini, vinginevyo itasubiri kwenda Nusu Fainali kwa miujiza.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA NI KUFA NA KUPONA LEO GHANA, VINGINEVYO NDIYO BASI TENA! Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top