• HABARI MPYA

    Friday, July 29, 2016

    KATIBU MKUU TFF AUNGURMA UFUNGUZI WA AIRTEL RISING STARS

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KATIBU Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Mwesigwa Selestine amesema kutimia kwa malengo ya Kampuni ya Simu za mkononi ya Airtel imesukuma kampuni hiyo kuendelea kudhamini mashindano ya soka kwa vijana - wavulana na wasichana.
    Selestine alisema hayo kwenye hafla ya kukabidhiana vifaa kwa Airtel kwenda TFF kabla ya kwenda kwa klabu shiriki iliyofanyika Ukumbi wa TFF, Dar es Salaam. Vifaa vilivyotolewa kwa timu jezi kamili ikiwa ni pamoja na jezi za waamuzi, viatu, mipira na vizuia ugoko kutopata madhara.
    Alisema sababu hizo ni uhusiano mzuri kati ya TFF na Airtel inayotoa bora za mawasiliano kwa miaka sita sasa sambamba na kuendeleza vipaji kwani nusu ya wachezaji wa timu ya taifa ya vijana wenye umri wa chini ya miaka 17, wanatoka katika michuano hiyo ya mwaka jana.
    Wachezaji hao ni  Ramadhani Awm Kabwili, Nickson Clement Kibabage, Dickson Nickson Job, Ally Hamisi Ng’anzi, Syprian Benedictor Mtesigwa, Mohammed Abdallah Rashid na Muhsin Malima Makame na Katibu Mkuu alisema: “Hawa wamepita Airtel. Tunashukuru Airtel kwa kuingia katika zonal (ukanda) ambao wengi hawapendi kuingia.”
    Selestine alisifu Airtel akisema imejitofautisha na taasisi nyingine na kuamua kwenda shambani au jikoni kulima au kupika chakula ambacho leo tunajivunia kuwa na kikosi bora na imara cha Serengeti Boys ambayo wiki ijayo itakuwa na mtihani dhidi ya Afrika Kusini.
    Rai ya Katibu Mkuu, Selestine ni kwa viongozi kuratibu vema mashindano ya Aitel msimu huu kwa kufuata kanuni ambazo zilijadiliwa na kupitishwa mara baada ya kuzindua mashindano hayo. “Kama viongozi mmeingia kwenye mashindano haya na hujafuata au hujui kanuni ujue tu umejiandaliwa kushindwa.”
    Kadhalika aliwataka wazazi na walezi kuwatia shime wachezaji ili wafanye vema kwenye michuano hii ili siku moja waingie kwenye ajira ya soka wakitokea mashindano ya kuibua vipaji ya Airtel. Pia alitaka wajitokeze kwa wingi kwenye mashindano hayo yatayosimamiwa na kuendeshwa na TFF katika mikoa mbalimbali.
    Mikoa ambayo itazindua Mashindano hayo ni pamoja na Mbeya, Mwanza, Morogoro, Ilala, Kinondoni na Temeke kwa upande wa wavulana wakati wasichana mikoa iliyoteuliwa ni Lindi, Zanzibar, Arusha na Ilala, Kinondoni na Temeke.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KATIBU MKUU TFF AUNGURMA UFUNGUZI WA AIRTEL RISING STARS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top