MABINGWA wa England, Leicester City wanakamilisha uhamisho wa Pauni Milioni 18 wa Ahmed Musa kutoka CSKA Moscow ya Urusi, baada ya Mnigeria huyo kutua kwa vipiko vya afya jana.
Nyota huyo mwenye umri wa miaka 23 anatarajiwa kutambulishwa wikiendi hii na kuungana na wachezaji wenzake wapya kwa kambi yao ya maandalizi ya msimu mpya nchini Austria wiki ijayo.
Musa atakuwa mchezaji wa nne kusajiliwa Leicester City baada ya Ron-Robert Zieler, Luis Hernandez na Nampalys Mendy.
Ahmed Musa yuko mbioni kutua Leicester kwa Pauni Milioni 18 kutoka CSKA Moscow PICHA ZAIDI GONGA HAPA
Mshambuliaji huyo amefunga mabao 13 na kutoa pasi za mabao matano kwa CSKA kwenye mechi 30 za Ligi Kuu ya Urusi alizocheza msimu wa 2015-2016 - ambayo ni mafanikio makubwa zaidi tangu ajiunge na kikosi cha Leonid Slutsky kutoka VVV-Venlo ya Uholanzi mwaka 2012.
Leicester ilijaribu bila mafanikio kumsajili Musa Januari mwaka huu. Musa alikuwa kwenye kambi ya mazoezi ya CSKA eneo la jeshi la nchi hiyo, umbali wa maili 10 kutoka Moscow akifanya mazoezi na wachezaji wenzake Jumamosi, lakini hakucheza mchezo wa kirafiki dhidi ya FC Yenisey Krasnoyarsk Jumapili.
Musa, ambaye anaweza kucheza kama winga na mshambuliaji amefunga jumla ya mabao 54 katika mechi 168 alizoichezea klabu hiyo ya Urusi na alianza kuichezea Super Eagles Septemba mwaka 2010 dhidi ya Madagascar.
Katika timu yake ya taifa ya Nigeria hadi sasa amefunga mabao 11 kwenye mechi 58 alizocheza, yakiwemo mawili katika ushindi wa 3-2 wa Super Eagles dhidi ya Argentina katika fainali za Kombe la Dunia mwaka 2014 nchini Brazil.
Wakati huo huo, CSKA Moscow imemsajili Lacina Traore kwa mkopo kuziba pengo la Musa anayekwenda Leicester.
0 comments:
Post a Comment