• HABARI MPYA

    Sunday, July 10, 2016

    AZAM YAWATEMA WANGA, MOURAD NA DIOUF....BEKI WA MEDEAMA NAYE 'ATIMULIWA'

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    UONGOZI wa Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati Azam FC, umetangaza rasmi kuwatema wachezaji sita kwa awamu ya kwanza huku nyota wawili wakifeli majaribio.
    Nyota hao walioachwa ni makipa Ivo Mapunda, Khalid Mahadhi aliyekuwa ametolewa kwa mkopo Mafunzo ya Zanzibar, mabeki Said Mourad, Racine Diouf kutoka Senegal pamoja na washambuliaji Didier Kavumbagu (Burundi) na Allan Wanga (Kenya).
    Ofisa Habari wa Azam FC, Jaffar Idd, amesema wachezaji hao wameachwa wakiwa wamepata stahiki zao kwa wale ambao waliokuwa wamebakiwa na mikataba.
    Said Mourad ameachwa Azam FC pamoja na Allan Wanga na Racine Diouf
    Alisema mbali na wachezaji hao, pia wachezaji wawili kati ya wanne waliokuwa kwenye majaribio nao wameachwa rasmi ambao ni beki wa kushoto kutoka Ghana, Nurudeen Yusif aliyetokea Medeama ya huko na kiungo mshambuliaji David Wirikom (Cameroon).
    Wawili hao wamepewa majibu ya kufeli majaribio yao leo asubuhi kufuatia Kocha Mkuu Zeben Hernandez, kutoridhishwa na uwezo wao kwa siku nne walizofanya mazoezi na kikosi cha Azam FC.
    “Wakati tunajiandaa na msimu mpya kuna wachezaji tuliwaalika kutoka nchi mbalimbali Afrika kwa ajili ya kufanya majaribio, ambao mpaka sasa wapo wanne, tangu tulipoanza mazoezi kwa siku takribani nne mwalimu leo ameamua kuwapunguza wawili na wawili wamebakia.
    “Waliofeli majaribio ni David Wirikom kutoka Cameroon na Nurudeen Yusif kutoka Ghana, kocha ameona viwango vyao havitofautiani sana na viwango vya wachezaji wetu hapa nyumbani, kocha ameongea nao leo mara baada ya mazoezi na kuwaambia haoni kama wanaweza kumsaidia kwa sababu anataka kuona mtu wa kimataifa anayekuja awe zaidi ya wachezaji wetu,” alisema.
    Wachezaji wanaoendelea kwenye majaribio ni makipa Daniel Yeboah (Ivory Coast) na Juan Jesus Gonzalez (Hispania), ambao wanawania nafasi moja ya usajili katika eneo la golikipa.
    Jaffar alimalizia kwa kusema kuwa wanatarajia kuwapokea wachezaji wengine wa kimataifa ndani ya siku mbili au tatu zijazo kwa ajili ya majaribio yote ni katika kuendelea.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM YAWATEMA WANGA, MOURAD NA DIOUF....BEKI WA MEDEAMA NAYE 'ATIMULIWA' Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top