TIMU ya Afrika Kusini imefanikiwa kutinga Hatua ya 16 Bora Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika baada ya ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Zimbabwe katika mchezo wa Kundi B leo Uwanja wa Marrakech Jijini Marrakech nchini Morocco.
Mabao ya Bafana Bafana yamefungwa na winga wa Orlando Pirates, Tshepang Moremi dakika ya saba, mshambuliaji wa Burnley ya England, Lyle Brent Foster dakika ya 50 na winga mwingine wa Orlando Pirates, Oswin Reagan Appollis.
Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa mwenyeji, Mustapha Kechchaf — mabao ya The Warriors yamefungwa na kiungo wa Motherwell ya Scotland, Tawanda Jethro Maswanhise dakika ya 19 na kiungo anayeweza kucheza kama beki wa pembeni pia, Aubrey "Postman" Modiba wa Mamelodi Sundowns aliyejifunga dakika ya 73.
Mechi nyingine ya Kundi B leo Angola imetoa sare ya bila mabao na Misri Uwanja wa Adrar mjini Agadir nchini Morocco zinakoendelea Fainali hizo za 35 za AFCON.
Kwa matokeo hayo, Misri inamaliza na pointi saba kileleni, ikifuatiwa na Afrika Kusini yenye pointi sita na zote zinasonga mbele zikiziacha Angola yenye pointi mbili na Zimbabwe yenye pointi moja.



.png)
0 comments:
Post a Comment