• HABARI MPYA

    Friday, May 18, 2018

    ZAHERA ASAINI MKATABA WA MIAKA MIWILI LEO JANGWANI KUPIGA KAZI YANGA

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    KOCHA Mwinyi Zahera kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), leo amesaini mkataba wa miaka miwili kuifundisha klabu ya Yanga ya Dar es Salaam baada ya wiki mbili za kuwa nchini.
    Kocha huyo Msaidizi wa timu ya taifa ya DRC, The Leopard mwenye uzoefu wa kufundisha soka hadi Ulaya, amesaini mkataba huo jioni ya leo makao ya klabu makutano ya mitaa ya Twiga na Jangwani Jijini Dar es Salaam.
    Na baada ya kusaini mkataba huo, Zahera anaondoka kurejea kwao, Kinshasa kwa ajili ya kuiandaa The Leopard kwa mchezo wa kirafiki dhidi ya Nigeria Uwanja wa Adokiye Amiesimaka mjini Port Harcourt Mei 28.
    Mwinyi Zahera amesaini mkataba wa miaka miwili leo kuifundisha klabu ya Yanga  

    Lakini Zahera ni kocha mzoefu aliyezifundisha pia DC Motema Pembe ya kwao, DRC tangu Machi 1, mwaka 2015 hadi Machi 10, 2016, akitoka kuwa kaimu kocha wa AFC Tubize ya Ubelgiji kati ya Oktoba 7 na Oktoba 23, mwaka 2014 ambayo alijiunga nayo akitoka kuwa Kocha Msaidizi wa timu ya taifa ya DRC kati ya Agosti 14 na 28, mwaka 2017 chini ya Ibenge.
    Alikuwa anafundisha AFC Tubize kwa mara ya pili, baada ya awali kuifundisha kama Kocha Mkuu kuanzia Julai 1 hadi Oktoba 20, mwaka 2010.
    Zahera Mwinyi alizaliwa Oktoba 19, mwaka 1962 kabla ya kuanza soka mwaka 1975 akiichezea klabu ya Bankin ya Goma, Kaskazini mwa jimbo la Kivu, DRC hadi mwaka 1980.
    Baadaye akaenda Kinshasa kucheza soka na kujiendeleza kielimu, akijiunga na Chuo cha Teknolojia (ISTA) huku akichezea klabu ya Sozacom hadi alipokutana na wakala wa wachezaji, Mbelgiji Karl Broken aliyemchukua na kumpeleka Ulaya kucheza soka ya kulipwa.
    Mwinyi Zahera alicheza kwa misimu miwili Antwerp FC ya Ubelgiji kabla ya kumaliza mkataba wake na kwenda Ufaransa alikochezea timu za Daraja la Pili, Amiens, Beauvais na Abbeville hadi akastaafu soka.
    Baada ya hapo akaanza kupata mafunzo ya ukocha, Zahera Mwinyi ambako alitunukiwa Diploma na leseni A ya Shirikisho la Soka Ulaya (UEFA) kabla ya kuifundisha klabu ya SC Feignies ya Ufaransa kuanzia mwaka mwaka 2000 hadi 2010 kwa mafanikio makubwa kabla ya kwenda Ubelgiji kuifundisha Tubize na baadaye jkutrejea nyumbani, DRC na sasa amekuja kujaribu maisha mapya Tanzania.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ZAHERA ASAINI MKATABA WA MIAKA MIWILI LEO JANGWANI KUPIGA KAZI YANGA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top