• HABARI MPYA

    Thursday, May 24, 2018

    SIMBA SC WAZAWADIWA MILIONI 100 NA SPORTS PESA KWA KUTWAA UBINGWA WA LIGI KUU

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KLABU ya Simba leo imezawadiwa kitita cha Sh. Milioni na wadhamini wao, kampuni ya SportPesa Tanzania kufuatia kutwaa taji la ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara msimu huu.
    SportPesa Tanzania, ambao pia ni wadhamini wa mahasimu wa Simba, Yanga imetekeleza kipengele cha mkataba wao kinachosema timu itakayotwaa ubingwa wa Ligi Kuu itapewa kiasi hicho cha fedha.
    Akizungumza na Waandishi wa Habari katika hafla ya kukabidhi fedha hizo iliyofanyika kwenye ofisi za Sports Pesa Tanzania, Oysterbay, Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Utawala na Udhibiti wa kampuni hiyo, Tarimba Abbas aliwapongeza viongozi na wachezaji wa Simba kwa kaz nzuri.
    Nahodha wa Simba SC, John Bocco 'Adebayor' akimkabidhi Kombe Mkurugenzi Mtendaji wa SportsPesa, Pavel Slavkov (kushoto) leo Oysterbay mjini Dar es Salaam 


    Mkurugenzi Mtendaji wa SportsPesa, Pavel Slavkov (kushoto) akimkabidhi mfano wa hundi ya Sh. Milioni 100 Nahodha wa Simba SC, John Bocco 'Adebayor' leo Oysterbay mjini Dar es Salaam 

    Tarimba, Rais wa zamani wa Yanga alisema kwamba ubingwa huo umewapa heshima kubwa wana Msimbazi na kubwa zaidi ni heshima waliyowapa wao kama wadhamini wao wakuu. 
    “Awali ya yote niwapongeze viongozi na wachezaji kwa ujumla kwa kupambana hadi kuweza kuchukua ubingwa wa Ligi kuu Tanzania bara msimu wa 2017/2018 na sisi kama wadhamini wenu wakuu tunatekeleza ile ahadi  tuliyoiweka kuwa Timu inayodhamiwa na Kampuni yetu itapewa Shilingi Milioni 100 na leo tumelitimiza hilo,”.
    “Simba imeitendea haki nembo yetu ya SportsPesa na Kampuni inaamini kuwa kwa SportsPesa kuwa wadhamini wakuu imekuwa nimoja ya chachu iliyosababisha Simba SC kuchukua ubingwa msimu huu" amesema Tarimba 
    Wakati huo huo; Tarimba amewataka Viongozi kupeleke kikosi kamili kwenye michuano ya SportsPesa Super Cup inayotarajia kuanza Juni 3 hadi 10 nchini Kenya, ili kuweza kufanya vizuri katika michuano hiyo kuwa Mabingwa na kurudi nyumbani na kitita cha dola za Kimarekani 30,000 pamoja na kupata nafasi ya kwenda nchini Uingereza kucheza na Everton FC ya Ligi Kuu ya England Uwanja wa Goodison Park. 
    Kwa upande wake Kaimu Makamu wa Rais wa Simba SC, Iddi Kajuna ameishukuru Kampuni ya SportsPesa kwa kuleta mabadiliko kwenye soka nchini ambayo wao kama klabu wameyaona kwa upande wao.
    “Moja ya mambo ambayo Simba inajivunia msimu huu ni kuwa na mdhamini kama SportsPesa, ambaye mbali na udhamini, pia tumekuwa tukishirikiana naye katika shughuli mbalimbali za kiuongozi, tulifanya maandalizi mazuri msimu huu kuanzia kwenye ngazi ya uongozi hadi benchi la ufundi na ndio maana siyo jambo la ajabu Simba kuchukua Ubingwa, kwani tulishaandaa mikakati ya kushinda kwa kushirikiana na wadhamini wetu" amesema Kajuna
    Simba SC ni miongoni mwa timu nne kutoka Tanzania zitakazoshiriki michuano ya SportsPesa Super Cup itakayofanyika nchini Kenya kuanzia Juni 3 hadi 10 ikishirikisha time nane kutoka nchini Tanzania na Kenya. 
    Timu nyingine ni pamoja na Yanga, Singida United na JKU ya Zanzibar, Gor Mahia, AFC Leopards, Kakamega Home Boys  na Kariabangi Sharks za Kenya. Gor Mahia ndiye bingwa mtetezi wa michuano hiyo baada ya kuwafunga watani wao wao jadi, AFC Leopard katika fainali mwaka jana Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC WAZAWADIWA MILIONI 100 NA SPORTS PESA KWA KUTWAA UBINGWA WA LIGI KUU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top