• HABARI MPYA

    Sunday, May 13, 2018

    NGORONGORO HEROES YACHAPWA 2-1 NA MALI NYUMBANI…AMMY NINJE ABEBESHWA LAWAMA KUMUWEKA BENCHI KABWILI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TANZANIA imejiweka kwenye mazingira magumu ya kusonga mbele katika mchujo wa kuwania tiketi ya Fainali za Vijana chini ya umri wa miaka 20 Afrika, baada ya kufungwa mabao 2-1 na Mali jioni ya leo Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.
    Tanzania, Ngorongoro Heroes sasa watalazimika kwenda kushinda ugenini kuanzia 2-0 Mei 20 mjini Bamako katika mchezo wa marudiano ili kuingia hatua ya mwisho ya mchujo wa kuwania tiketi ya Niger mwakani.
    Katika mchezo huo uliochezeshwa na marefa kutoka Comoro, Soulaimane Ansudane aliyepuliza kipyenga akisaidiwa na washika vibendera Mmadi Faissoil na Abdoulmadjid Azilani, hadi mapumziko tayari Mali walikuwa mbele kwa mabao 2-1.
    Ousmane Diakite alianza kuifungia Mali dakika ya 37 akitumia makosa ya kipa wa Ngorongoro Heroes, Abdultwali Msheri kupiga mpira bila uangalifu, ambao ulinaswa na wapinzani na kufunga.
    Kipa wa Ngorongoro Heroes, Abdultwalib Msheri akiwa chini baada ya Mali kupata bao la kwanza
    Mfungaji wa bao la pili la Mali, Samadiare Dianka akitafuta maarifa ya kuwapita wachezaji wa Ngorongoro
    Hivi ndivyo namna ambavyo Ngorongoro walifungwa bao la pili

    Wakati Ngorongoro Heroes wanahangaika kutafuta bao la kusawazisha, wakajikuta wakichapwa bao la pili rahisi kwa makosa ya kipa tena, mfungaji Samadiare Dianka kwa shuti la mpira wa adhabu.
    Msheri alikwenda kusimama nyuma ya ukuta wa wachezaji wake na kumrahisishia Dianka kazi kwa kuupeleka mpira upande uliokuwa wazi, kushoto kwa mlinda mlango huyo.
    Mshambuliaji chipukizi wa Azam FC, Paul Peter akaifungia Ngorongoro Heroes bao la kufutia machozi dakika ya 44 akiuwahi mpira uliotemwa na kipa wa Mali, Youssouf Keita kufuatia shuri la mpira wa adhabu.
    Kipindi cha pili mvua iliyoanza kunyesha tangu asubuhi ikaongezeka na ladha ya mpira ikapungua kutokana na uwanja kuwa unateleza na haikuwa ajabu matokeo hayakubadilika.
    Kipigo cha leo lawama zinakwenda kwa Kocha Mkuu, Ammy Ninje ambaye  hakumpanga kipa namba moja, Ramadhani Kabwili ambaye alitofautiana naye kabla ya mchezo wa leo.
    Ninje alikasirishwa na kitendo cha Kabwili kwenda na klabu yake, Yanga nchini Algeria kwenye Kombe la Shirikisho bila kuaga na akamfukuza kwenye timu.  
    Lakini Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wallace Karia akamrejesha kipa huyo kikosini, akisema kilichotokea ni kukosekana kwa mawasiliano mazuri baina ya klabu ya Kabwili na uongozi wa timu na shirikisho.
    Kabwili alikuwa namba moja wa timu ya vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys iliyoshiriki fainali za U17 za Afrika nchini Gabon Mei mwaka jana, ambayo wachezaji wake wengi ndiyo wanaunda Ngorongoro.
    Na ndiye aliyedaka mechi zote mbili Ngorongoro ikiitoa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) katika Raundi ya Kwanza kwa penalti 6-5 mjini Kinshasa baada ya sare mbili za 0-0 nyumbani na ugenini,  kabla ya kwenda kuokoa penalti kwenye mechi ya marudiano na kuivusha Ngorongoro hadi hatua hii.     
    Mshindi wa jumla atakutana na mshindi kati ya Cameroon na Uganda katika hatua ya mwisho ya mchujo.
    Kikosi cha Ngorongoro Heroes kilikuwa; Abdultwali Msheri, Israel Mwenda, Nickson Kibabage, Ally Msengi, Dickson Job, Enrick Nkosi/Shaaban Ada dk57, Said Mussa, Asad Juma/Kelvin Nashon dk54, Paul Peter, Habib Kiyombo na Abdulnasir Bitebo/Muhsin Makame dk70.
    Mali; Youssouf Keita, Abdoulaye Diaby, Dante Amadou, Kanoute Clement, Fode Konate, Mamady Diara/Hadji Drame dk51, Mamadou Samake, Ousmane Diakite, Samadiare Dianka, Traore Mamadou na Amadou Diara/ Gary Moussa dk64/Falaye Keita dk90+3.

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NGORONGORO HEROES YACHAPWA 2-1 NA MALI NYUMBANI…AMMY NINJE ABEBESHWA LAWAMA KUMUWEKA BENCHI KABWILI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top