• HABARI MPYA

    Saturday, January 16, 2016

    SAMATTA ‘AMLIZA’ RAIS WA NANTES YA UFARANSA, KUMBE MBWANA AMEKWISHASAINI GENK…NA KATUMBI SASA ATAKA EURO MILIONI KUMUACHA, VINGINEVYO ARUDI LUBUMBASHI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    RAIS wa klabu ya Nantes ya Ufaransa,
    Mbwana Samatta (kushoto) anasubiriwa Ufaransa akasaini Nantes ya Ligi Kuu, lakini mwenyewe anataka kwenda KRC Genk ya Ubelgiji
    Waldemar Kita amesikitishwa mno na kitendo cha mshambuliaji wa kimataifa wa Tanzania, Mbwan Ally Samatta kukataa ofa ya kujiunga na klabu yake, lakini hajakata tamaa kwa sababu kijana huyo bado ni mali ya TP Mazembe.

    “Tungependa kumpata. Inavyoonekana amesaini (KRC Genk). Lakini ni mali ya klabu gani? Atakuwa huru mwishoni mwa msimu? Mawakili wangu wanalishughulikia hilo suala kwa siku mbili, au tatu,”. 
    “Kama itakuwa poa, au hapana, vizuri, mbaya sana, yote maisha,” amesema katika safu ya Ocean Press.
    Wakati huo huo, tovuti ya Gazeti la Lequipe la Ufaransa limeandika, Samatta mwenye umri wa miaka 24 sasa, amekwishasaini Mkataba wa awali na KRC Genk ya Ubelgiji. 
    Na lakini akiwa na Mkataba na TP Mazembe hadi Aprili 30, Mwanasoka huyo Bora Anayecheza Afrika hawezi kuruhusiwa kwa dau la chini ya Euro Milioni 1.
    Na wakati Samatta tayari amepatiwa viza na Ubalozi wa Ubelgiji kwenda kusaini klabu ya KRC Genk, Rais wa Mazembe, Moise Katumbi amegoma kusikikiliza kuhusu klabu hiyo ya Ligi Kuu ya Ubelgiji.

    Rais wa Nantes ya Ufaransa, Waldemar Kita amesikitishwa na Samatta kukataa ofa ya kujiunga na klabu yake

    BIN ZUBEIRY SPORTS – ONLINE inafahamu Katumbi anataka Samatta aende Nantes FC ya Ligi Kuu ya Ufaransa, ambayo amekwishafikia makubaliano nayo.
    Na wiki iliyopita Nantes FC ilituma mwakilishi wake Dar es Salaam, ambaye alifanya mazungumzo na Meneja wa Samatta, Jamal Kisongo mbele ya Ofisa mmoja wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
    Katika mazungumzo, Kisongo alifikia makubaliano ya maslahi binafsi na Samatta ikiwemo dau la kusaini, mshahara, masharti na marupurupu mengine.
    Kisongo alitaka kiwepo kipengele cha mchezaji kutorejeshwa Afrika iwapo hatapata nafasi ya kucheza Nantes, bali auzwe klabu nyingine ya Ulaya na ikakubaliwa.
    Nantes ilionyesha nia ya dhati kabisa ya kumchukua Samatta na Kisongo aliinuka kwenye meza ya mazungumzo akiwa amekubali na kusema anakwenda kuzungumza na mchezaji.
    Hata hivyo, inaonekana Samatta mwenyewe ndiye anayetaka kwenda Ubelgiji na si Ufaransa, kwani kitendo cha Kisongo kutorejesha majibu kwa Nantes kinaashiria ameshindwa kumshawishi mchezaji wake akubali ofa hiyo.
    Wakati huo huo, Rais wa Mazembe hayuko tayari kumuuza Samatta Ubelgiji na yuko tayari kuona Samatta anabaki Mazembe kumalizia Mkataba wake ili aondoke kama mchezaji huru Aprili, hali ambayo itamlazimu kusubiri hadi Agosti kusaini Genk.
    Moise Katumbi hayuko tayari kumruhusu Samatta kwenda KRC Genk, bali anataka aende Nantes

    Kwa sasa, kambi ya Samatta inajaribu kuomba msaada kwa viongozi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wakazungumze na Katumbi ili akubali kumuacha mchezaji aende klabu aliyochagua.
    Rais Mstaafu, Dk Jakaya Mrisho Kikwete ambaye kwa sasa ni Mwenyekiti wa chama tawala, CCM, Waziri wa Michezo, Nape Nnauye kwa pamoja wameahidi kumsaidia Samatta katika suala la kumlainisha Katumbi akubali kupokea ofa ya Genk.
    Wakati huo huo, Nantes wamekuwa wakimpigia simu Kisongo wakisema wanamsubiri mchezaji aende kusaini, lakini Meneja huyo anakosa majibu ya uhakika.
    Inaonekana tayari Katumbi anaujua mchezo wote unaoendelea naye ameamua kukaa kimya akiamini Samatta hawezi kufanya chochote kwa sasa bila baraka zake. 
    Watamsaidia? Rais Mstaafu, Dk Jakaya KIkwete (kushoto) na Waziri wa Michezo, Nape Nnauye (kulia) wakiwa na Samatta katikati

    Na wazo la kusema Samatta asubuhi hadi Aprili atakapomaliza Mkataba wake ili asaini kama mchezaji huru Agosti halifurahiwi hata na Kisongo mwenyewe.
    Samatta aliyejiunga na TPM mwaka 2011 akitokea Simba SC aliyoichezea kwa nusu msimu, akitokea African Lyon, hadi sasa ameichezea klabu hiyo mechi 103 na kuifungia mabao 60.
    Ndani ya mechi hizo, kijana huyo wa umri wa miaka 24, ameshinda taji la Ligi ya Mabingwa Afrika na Mazembe, huku naye akiibuka mfungaji bora wa michuano hiyo na kutwaa tuzo ya Mchezaji Bora Anayecheza Afrika.   
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA ‘AMLIZA’ RAIS WA NANTES YA UFARANSA, KUMBE MBWANA AMEKWISHASAINI GENK…NA KATUMBI SASA ATAKA EURO MILIONI KUMUACHA, VINGINEVYO ARUDI LUBUMBASHI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top