• HABARI MPYA

    Wednesday, January 20, 2016

    SUGIRA AIPELEKA RWANDA ROBO FAINALI CHAN, YAIBABUA 2-1 GABON

    MABAO mawili ya Ernest Sugira yameipa ushindi wa pili mfululizo Rwanda katika mchezo wa Kundi A Michuano ya Ubingwa wa Mataifa ya Afrika (CHAN), inayohusisha wachezaji wanaocheza ligi za nchini mwao pekee kufuatia ushindi wa 2-1 dhidi ya Gabon leo.
    Katika mchezo huo uliofanyika Uwanja wa Amahoro, Kigali – Sugira alifunga mabao hayo dakika za 42 akimalizia pasi ya Jacques Tuyisenge na dakika ya 47 akiunganisha pasi ya Dominique Nshuti.
    Ernest Sugira amefunga mabao yote mawili, Rwanda ikiilaza 2-1 Gabon na kutinga Robo Fainali CHAN

    Bao pekee la Gabon waliotoa sare ya 0-0 na Morocco katika mchezo wa kwanza, limefungwa na Aaron Boupendza dakika ya 55 akimalizia kazi nzuri ya Stevy Nzambe.
    Mchezo mwingine wa kundi hilo leo, bao pekee la penalti la Krahire Yannick Zakri dakika ya 10 limeipa Ivory Coast ushindi wa 1-0 dhidi ya Morocco.
    Sasa Rwanda inajihakikishia kwenda Robo Fainali kuelekea mechi yake ya mwisho ya kundi hilo dhidi ya Morocco, baada ya kufikisha pointi sita kutokana na mechi mbili, ikiongoza Kundi A ikifuatiwa na Ivory Coast yenye pointi tatu.
    Ivory Coast inaweza kufikisha pointi sita ikishinda mechi ya mwisho dhidi ya Gabon, wakati Morocco na Gabon hata zikishinda zitamaliza na pointi nne – hivyo haziwezi kuwazuia Rwanda kwenda Robo Fainali.   
    Michuano hiyo itaendelea kesho kwa mechi za Kundi B, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo DRC ikimenyana na Angola na Cameroon na Ethiopia Uwanja wa Huye.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SUGIRA AIPELEKA RWANDA ROBO FAINALI CHAN, YAIBABUA 2-1 GABON Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top