• HABARI MPYA

    Tuesday, January 12, 2016

    NYOTA MTIBWA SUGAR ASEMA; “TUTALALA NAO MBELE HAO URA”

    ORODHA YA MABINGWA KOMBE LA MAPINDUZI
    Mwaka    Bingwa Mshindi wa Pili
    2007 Yanga SC Mtibwa Sugar 
    2008 Simba SC Mtibwa Sugar
    2009 Miembeni         KMKM
    2010 Mtibwa Sugar Ocean View
    2011 Simba SC   Yanga SC
    2012 Azam FC         Simba SC
    2013 Azam FC   Tusker FC
    2014 KCCA       Simba SC
    2015 Simba SC Mtibwa Sugar
    Kiungo tegemeo wa Mtibwa Sugar, Shizza KIchuya amesema watapigana kiume kesho wabakishe Kombe nyumbani

    Na Prince Akbar, ZANZIBAR
    KIUNGO tegemeo wa Mtibwa Sugar, Shizza Kichuya amesema kwamba wapinzani wao URA katika fainali ya Kombe la Mapinduzi ni wazuri, lakini watapigana kiume kuhakikisha wanabakisha taji hilo nyumbani.
    Kichuya anayeng’ara na Mtibwa Sugar katika michuano hii, kiasi cha kuzitamanisha timu kadhaa zikiwemo Azam, Simba na Yanga amesema kwamba mchezo wa kesho utakuwa mgumu, lakini watapambana kwa uwezo wao wote ili washinde.
    “Tunafahamu kwa sasa matumaini ya Watanzania yapo kwetu sisi ili tuweze kubakisha Kombe hili nyumbani, baada ya ndugu zetu wote kutolewa. Na kwa kutambua hilo, sisi kama wachezaji tutajituma,”amesema.
    Mtibwa Sugar inakutana na URA ya Uganda katika Fainali ya Kombe la Mapinduzi kesho usiku Uwanja wa Amaan, Zanzibar baada ya kuwatoa waliokuwa mabingwa watetezi, Simba SC Jumapili kwa kuwafunga 1-0.
    URA imefika katika mechi ya mwisho ya Kombe la Mapinduzi, baada ya kuwatoa mabingwa wa Tanzania Bara, Yanga SC kwa penalti 4-3 kufuatia sare ya 1-1 ndani ya dakika 90.
    Hii itakuwa mara ya tano kwa Mtibwa Sugar kufika fainali, baada ya awali kucheza fainali nne na kutwaa taji mara moja, 2010 ilipoifunga Ocean View ya hapa.
    Mtibwa iliingia fainali mwaka 2007 na kufungwa na Yanga SC – wakati 2008 na 2015 ilifungwa na Simba SC mara zote.
    URA ambao wanacheza mashindano haya kwa mara ya pili, hawajawahi kufika fainali, lakini mwaka 2014 taji la Mapinduzi lilipanda ndege kwenda Uganda, lilipochukuliwa na KCCA walioifunga Simba SC katika fainali.

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NYOTA MTIBWA SUGAR ASEMA; “TUTALALA NAO MBELE HAO URA” Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top