• HABARI MPYA

    Sunday, February 24, 2019

    YANGA SC YATINGA ROBO FAINALI KOMBE LA TFF BAADA YA KUITOA NAMUNGO RUANGWA

    Na Mwandishi Wetu, RUANGWA
    VIGOGO, Yanga SC wamefanikiwa kuingia Robo Fainali ya michuano ya Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu kama Azam Sports Federation Cup (ASFC) baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya Namungo FC jioni ya leo Uwanja wa Kassim Majaliwa wilayani Ruangwa mkoani Lindi.
    Shujaa wa Yanga SC kwa mara nyingine amekuwa mshambuliaji wake, Heritier Ebenezer Makambo raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) aliyefunga bao hilo pekee dakika ya 82 kwa kichwa cha kuparaza akimalizia krosi ya kiungo Deus Kaseke kutoka upande wa kulia.


    Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Abubakar Mturo aliyesaidiwa na washika vibendera Khalfan Sika na Kassim Safisha, Namungo FC walifanikiwa vizuri kuibana Yanga kipindi cha kwanza. 
    Na kipindi cha Yanga ilikianza na mabadiliko, kocha Mkongo Mwinyi Zahera akimpumzisha beki wa kushoto mwinyi Hajji Mngwali na Gardiel Michael Mbaga.
    Na hiyo ni baada ya Mngwali kunusurika kutolewa kwa kadi nyekundu dakika ya 43 baada ya kucheza rafu aliyostahili kuonyeshwa kadi ya njano akiwa tayari ameonyeshwa kadi hiyo awali, lakini refa Mturo akamuacha. 
    Namungo FC ilipoteza nafasi nzuri ya kupata bao dakika ya 60 baada ya mshambuliaji wake, Reliant Lusajo kumpelekea mpira mkononi kipa Mkongo, Klaus Kindoki akiwa kwenye boksi baada ya pasi ya kutanguliwa na mtokea benchi, Kelvin John.
    Dakika ya 76 Hashim Manyanya naye akafumua shuti kali akiwa umbali wa mita 18, lakini kipa Kindoki aliyekuwa katika ubora leo, akapangua ikatoka nje.
    Kikosi cha Namungo FC kilikuwa; Adam Oseja, Miza Chirtom, Jukumu Kibanda, Freddy Mlelwa, Hamisi Fakhi, Daniel Joram, Hashim Manyanya, John Mbise, Ramadhani Hussein/Abeid Athumani dk73, Lucas Kikoti/Kelvin John dk60 na Reliants Lusajo.
    Yanga SC; Klaus Kindoki, Paul Godfrey, Mwinyi Mngwali/Gardiel Michael dk46, Andrew Vincent ‘Dante’, Abdallah Shaibu ‘Ninja’, Feisal Salum, Mrisho Ngassa/Amissi Tambwe dk73, Papy Kabamba Tshishimbi, Heritier Makambo, Mohammed Issa ‘Banka’ na Ibrahim Ajibu/Deus Kaseke dk59.
    Mechi nyingine za ASFC leo, African Lyon imeitoa Mbeya City kwa penalti 4-3 kufuatia sare ya 2-2 ndani ya dakika 90 Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam, wakati Alliance FC imeifunga Dar City 3-0 Uwanja wa Nyamagana mjini Mwanza.
    Timu nyingine zilizotinga Robo Fainali ni Singida United iliyoitoa Coastal Union, KMC iliyowatoa waliokuwa mabingwa watetezi, Mtibwa Sugar, Kagera Sugar iliyoitoa Boma FC na Lipuli FC iliyoitoa Dodoma FC.

    Mechi ya kukamilisha hatua ya 16 Bora ya michuano hiyo itafanyika kesho Uwanja wa Azam Complex, Chamazi mjini Dar es Salaam. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC YATINGA ROBO FAINALI KOMBE LA TFF BAADA YA KUITOA NAMUNGO RUANGWA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top