• HABARI MPYA

    Wednesday, February 20, 2019

    TANZANIA PRISONS YAICHAPA MBEYA CITY 1-0, SINGIDA UNITED WAPIGWA 2-0 NANGWANDA

    Na Mwandishi Wetu, MBEYA
    BAO pekee la Salum Kimenya dakika ya 70, limeipa Tanzania Prisons ushindi wa 1-0 dhidi ya mahasimu wao wa Jiji, Mbeya City katika mchezo uliofanyika Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya.
    Kwa ushindi huo, Tanzania Prisons inafikisha pointi 32 baada ya kucheza mechi 27, ikijiinua hadi nafasi ya 12 kutoka ya 17, wakati Mbeya City inayobaki na pointi zake 30 baada ya kucheza mechi 25, inashuka kwa nafasi moja hadi ya 15.   
    Mechi nyingine za Ligi Kuu leo, bao pekee la Sadallah Lipangile dakika ya pili tu limeipa ushindi wa 1-0 KMC dhidi ya Mtibwa Sugar ya Morogoro Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam. 
    KMC inafikisha pointi 40 baada ya kucheza mechi 27 na kurudi nafasi ya nne, nyuma ya Simba SC yenye pointi 42 za mechi 17, Azam FC pointi 50 za mechi 24 na Yanga SC pointi 61 za mechi 25, wakati Mtibwa Sugar inayobaki na pointi zake 29 za mechi 23, inashuka kwa nafasi mbili hadi ya 17 kwenye ligi ya timu 20.

    Nayo Ndanda SC imeichapa Singida United 2-0 mabao ya Vitalis Mayanga dakika ya tisa na Mohamed Mkopi dakika ya 81 Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara.
    Ndanda FC inajiinua hadi nafasi ya 13 kutoka ya 18 ikifikisha pointi 32 baada ya kucheza mechi 26, wakati Singida United inayobaki na pointi zake 29 katika mechi ya 25, inashuka kwa nafasi mbili hadi ya 18.
    Nayo Stand United imeibuka na ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Lipuli FC ya Iringa Uwanja wa CCM Kambarage mjini Shinyanga.
    Mabao ya Stand United yamefungwa na Mourice Mahela dakika ya 33, Datus Peter dakika ya 59 na Nahodha Jacob Masawe dakika ya 90 na ushei, wakati ya Lipuli FC yamefungwa na Paul Nonga dakika ya 28 na Jimmy Shoji dakika ya 72.
    Kwa ushindi huo, Stand United inapanda hadi nafasi ya 10 kutoka ya 14, ikifikisha pointi 33 katika mechi ya 28, wakati Lipuli FC inashuka kwa nafasi moja hadi ya tano, ikibaki na pointi zake 38 baada ya kucheza mechi 27.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TANZANIA PRISONS YAICHAPA MBEYA CITY 1-0, SINGIDA UNITED WAPIGWA 2-0 NANGWANDA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top