• HABARI MPYA

    Wednesday, February 27, 2019

    IDDI CHECHE AFICHUA SIRI YA MAFANIKIO YAKE KILA AKIPEWA MAJUKUMU AZAM FC

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KOCHA wa muda wa Azam FC, Idd Nassor Cheche, amefunguka kuwa jambo kubwa linalombeba kila akikabidhiwa timu hiyo, ni kutokana na kuifahamu vema na kutopenda masikhara.
    Cheche anayesaidiana na Meja Mstaafu, Abdul Mingange, wote wakiwa makocha wa timu za vijana za Azam FC, wameshika nafasi hizo kwa muda baada ya kusitishiwa mikataba kwa Hans Van Der Pluijm na Msaidizi wake, Juma Mwambusi.
    Wawili hao waliiongoza Azam FC juzi usiku kuichapa Rhino Rangers mabao 3-0 na kutinga robo fainali ya michuano ya Kombe la Shirikisho (Azam Sports Federation Cup), mabao yakiwekwa kimiani na kiungo mshambuliaji Tafadzwa Kutinyu, kiungo Salum Abubakar ‘Sure Boy’ na mshambuliaji Obrey Chirwa.
    Idd Nassor Cheche (kulia) akiwa na Meja Mstaafu, Abdul Mingange kwenye mechi dhidi ya Rhino Rangers juzi

    Cheche amesema kwa sasa walichofanikiwa ni kunyanyua ari za wachezaji na kuwajenga kisaikolojia jambo ambalo limepelekea ushindi huo mnono.
    “Mimi huwa ni mshindani, napenda kushindana, sipendi kupoteza, ninapopata nafasi ya kuishika timu huwa sipendi masikhara, kingine naifahamu vizuri Azam FC wachezaji wengi nawajua, nawapongeza vijana kwa kazi nzuri na kubwa waliyofanya na kupata ushindi huu muhimu,” alisema.
    Kocha huyo mwenye ushawishi mkubwa ndani ya viunga vya Azam Complex, aliwaomba mashabiki wa timu hiyo kuwapa ushirikiano kwa kipindi hiki kifupi walichokuwa na timu hiyo.
    “Nawaahidi mambo mazuri yanakuja kama walivyonizoea, cha muhimu ni mashabiki kutupa ushirikiano kwa kujaa kwa wingi uwanjani na kuisapoti timu pia, hata pale atakapokuwa amepatikana kocha mpya,” alisema.
    Mara baada ya mchezo huo, Azam FC inaelekeza nguvu zake zote kwenye mchezo ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara (TPL) dhidi ya African Lyon, utakaofanyika Ijumaa hii.
    Mabingwa hao, sasa wamerejea kwenye mwendo wa ushindi ambapo kwa kutoa dozi hiyo kunawafanya kupata ushindi wa kwanza tokea kuanza kwa mwezi huu Februari katika mechi sita ilizocheza.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: IDDI CHECHE AFICHUA SIRI YA MAFANIKIO YAKE KILA AKIPEWA MAJUKUMU AZAM FC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top