• HABARI MPYA

    Tuesday, August 01, 2017

    HASSAN ISIHAKA ATUA MTIBWA SUGAR BAADA YA KUMALIZANA NA SIMBA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MABINGWA wa zamani wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Mtibwa Sugar wameendeela kujiimarisha kuelekea msimu ujao baada ya kumsajili beki wa zamani wa Simba SC, Hassan Suleiman Isihaka.
    Timu hiyo inayomilikiwa na kiwanda cha Sukari bora nchini Mtibwa Sugar kilichopo mkoani Morogoro, imefanikiwa kunasa saini ya beki huyo ambaye msimu uliopita aliichezea kwa mkopo African Lyon ya Dar es Salaam.
    Hata hivyo, baada ya African Lyon kuteremka Daraja msimu uliopita, Isihaka akafikia makubaliano maalum ya kuvunja mkataba na Simba ili awe huru na hivyo kufanikiwa kujiunga na Mtibwa Sugar.
    Hassan  Isihaka ametua Mtibwa Sugar ya Morogoro kutoka African Lyon alipokuwa anacheza kwa mkopo kutoka Simba, zote za Dar es Salaam 

    Ujio wa beki huyo ni pendekezo la benchi la ufundi la Mtibwa Sugar linaloongozwa na Zuberi Katwila.
    “Kiukweli usajili huu niliusubilia kwa hamu yote kubwa nadhani kila kocha anatamani kuwa na mchezaji huyu nadhani bahati imedondokea kwa Mtibwa Sugar , pia natoa shukrani za dhati kwa viongozi kwa kufanikisha usajili huu maana ulikua wa muhimu sana kwangu,” amesema Katwila.
    Kwa upande wake. Isihaka amesema kwamba alikua anatamani kufanya kazi na 'Wana Tam Tam' kwa muda mrefu; “Nilikua natamani kufanya kazi na Mtibwa Sugar kwa muda mrefu na ninadhani nimefanikiwa kwa kuwa ni klabu kubwa na wachezaji wengi nchini wakubwa wamepita hapa,” amesem Isihaka.
    Isihaka anakuwa mchezaji mpya wa saba kusajiliwa na Mtibwa Sugar dirisha hili, wengine wakiwa ni kipa Shaaban Hassan Kado, mabeki Salum Kanoni kutoka Mwadui, Hussein Idd Hante kutoka JKT Oljoro, viungo Hassan Dilunga kutoka JKT Ruvu na washambuliaji ni Riffat Khamis Msuya kutoka Ndanda FC na Salum Ramadhani Kihimbwa 'Chuji'.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HASSAN ISIHAKA ATUA MTIBWA SUGAR BAADA YA KUMALIZANA NA SIMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top