• HABARI MPYA

    Wednesday, August 30, 2017

    EMMANUEL MARTIN AONGEZWA TAIFA STARS

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    KOCHA wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Salum Shaaban Mayanga amemuongeza kwenye kikosi cha timu hiyo, winga Emmanual Martin wa Yanga.
    Martin aliyejiunga na Yanga SC dirish dogo msimu uliopita kutoka KMKM ya Zanzibar anatarajiwa kujiunga na Stars kambini leo mjini Dar es Salaam kuendelea na maandalizi ya mchezo wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya Botswana Jumamosi.
    Stars imeweka kambi katika hoteli ya Sea Scape iliyoko Kunduchi, Dar es Salaam huku ikiendelea na mazoezi Uwanja wa Taifa.
    Wachezaji wengine waliopo kambini ni makipa Aishi Manula (Simba SC), Mwadini Ally (Azam FC) na Ramadhani Kabwili (Yanga SC).
    Mabeki ni Gardiel Michael (Yanga SC), Boniphas Maganga (Mbao FC), Abdi Banda (Baroka FC/Afrika Kusini), Kelvin Yondani (Yanga SC), Salim Mbonde (Simba SC) na Erasto Nyoni (Simba SC).
    Viungo ni Himid Mao (Azam FC), Hamis Abdallah (Sony Sugar/Kenya), Mzamiru Yassin (Simba SC), Said Ndemla (Simba SC), Simon Msuva (Difaa El Jadidah/Morocco), Shiza Kichuya (Simba SC), Farid Mussa (CD Tenerife/Hispania) na Orgenes Mollel (FC Famalicao/Ureno).
    Washambuliaji ni Raphael Daudi (Yanga SC), Kelvin Sabato (Azam FC), Mbwana Samatta (KRC Genk/Ubelgiji) na Elias Maguli (Dhofar FC/Oman).
    Benchi la Ufundi la Mayanga linaundwa na yeye mwenyewe ambaye ni Kocha Mkuu, Fulgence Novatus (Kocha Msaidizi), Patrick Mwangata (Kocha wa Makipa), Danny Msangi (Meneja), Dkt. Richard Yomba (Daktari wa timu), Dkt. Gilbert Kigadye (Daktari wa Viungo) na Ally Ruvu (Mtunza Vifaa).
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: EMMANUEL MARTIN AONGEZWA TAIFA STARS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top