• HABARI MPYA

    Thursday, August 31, 2017

    AZAM FC YAWAONGEZA MIKATABA AGGREY MORRIS NA SURE BOY

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    NYOTA wawili wa Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati Azam FC, nahodha msaidizi Aggrey Morris na Salum Abubakar ‘Sure Boy’ leo wameongeza mwaka mmoja wa kuendelea kuitumikia timu hiyo.
    Zoezi la kuingia mikataba hiyo lilisimamiwa na Makamu Mwenyekiti wa Azam FC, Abdulkarim Amin ‘Popat’, kwenye Ofisi za timu hiyo Mzizima, zilizopo Barabara ya Nyerere, Dar es Salaam.
    Awali mikataba yao ilitarajiwa kuisha mwishoni mwa msimu huu, hivyo kwa kuongeza mikataba mipya, itawafanya wachezaji hao kusalia ndani ya viunga vya Azam Complex hadi mwaka 2019.
    Uongozi wa Azam FC kwa kushirikiana na benchi la ufundi umewaongeza mikataba mipya wachezaji hao, kutokana na viwango vyao bora na mchango mkubwa wanaoendelea kuutoa ndani ya kikosi hicho.
    Makamu Mwenyekiti wa Azam FC, Abdulkarim Amin ‘Popat’ (kushoto) akimsainisha mkataba Salum Abubakar 'Sure Boy' 
    Wawili hao wapo muda mrefu Azam FC, Sure Boy akianzia kuichezea Azam FC tokea timu hiyo ilipokuwa madaraja ya chini kabla ya kupanda nayo Ligi Kuu mwaka 2008 huku Moris akijiunga na mabingwa hao mwaka 2009 akitokea Mafunzo ya Zanzibar.
    Wakati huo huo: WINGA wa kushoto wa Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati Azam FC, Joseph Kimwaga, anatarajiwa kuondoka nchini muda wowote kuanzia sasa kuelekea Afrika Kusini kufanyiwa upasuaji wa goti lake la mguu wa kushoto.
    Kimwaga aliteguka goti lake hilo Alhamisi iliyopita kwenye Uwanja wa Chuo cha Ualimu cha TTC cha mkoani Mtwara, wakati Azam FC ikijiandaa na mchezo wa kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) dhidi ya Ndanda ulioisha kwa mabingwa hao kushinda bao 1-0 wikiendi iliyopita.
    Daktari wa Azam FC, Mwanandi Mwankemwa amesema kwamba awali mchezaji huyo ilibidi afanyiwe kipimo cha MRI lakini ilishindikana kutokana na Kimwaga kuwahi kuwekewa kipande cha madini (metal) huku nyuma alipokuwa amekatika ‘ligament’ ya kati kwenye goti lake hilo.
    “Kwa hiyo kipimo cha MRI hakikuweza kufanyika, kilichofanyika ni ‘Ultra Sound’, ambayo ilithibitisha kwamba ndani ya goti lake kuna maji mengi na damu nyingi,” alisema.
    Mwankemwa alisema matibabu yake yapo ya aina mbili, ya kwanza ni kumfanyia upasuaji wa goti ili kuweza kujua tatizo ni nini na kuweza kutibu, ambapo kwa matibabu hayo itamfanya Kimwaga kurejea uwanjani baada ya miezi tisa.
    “Matibabu kwa njia ya pili ni kumfanyia ‘Arthroscopic’, ambacho ni kipimo maalum kinachofanya mambo mawili kinaweza kugundua tatizo na vilevile kikafanya matibabu, mapendekezo ni kwamba ilikuwa ni lazima akafanyiwe kipimo hiki kwani itamchukua miezi miwili tu kurejea dimbani,” alisema.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM FC YAWAONGEZA MIKATABA AGGREY MORRIS NA SURE BOY Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top