• HABARI MPYA

    Wednesday, August 30, 2017

    KESI YA AVEVA, KABURU YAPIGWA KALENDA TENA, WARUDISHWA RUMANDE

    Na Rehema Lucas, DAR ES SALAAM
    KESI inayowakabili viongozi viongozi wa klabu ya Simba, Rais Evans Elieza Aveva na Makamu wake, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ imeahirishwa tena kwa mara ya saba hadi  Septemba 8, mwaka huu.
    Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Dar es Salaam, Victoria Nongwa amesema leo mahakamani hapo kwamba ameiahirisha kesi hiyo ili kupisha uchunguzi wa nyaraka zilizokusanywa.
    Hakimu huyo amewataka mawakili wa upande wa Serikali kufanye haraka  kufuatilia nyaraka zilizokusanywa, ili kesi hiyo ianze kusikilizwa.
    Aveva na Kaburu wanakabiliwa na mashitaka matano yakiwemo ya utakatishaji fedha, ambayo hayana dhamana na wote wapo rumande gereza la Keko tangu Juni 29.
    Wawili hao leo waliletwa tena Mahakama ya Hakimu Mkazi, Kisutu, Dar es Salaam kwa mara ya saba tangu Takukuru ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU) iwatie hatiani na kusomewa tena mashitaka hayo kabla ya Hakimu Victoria Nongwa kuiahirisha tena kesi hiyo hadi Agosti 16, mwaka huu.
    Miongoni mwa mashitaka yanayowakabili ni pamoja na kughushi nyaraka zinazodaiwa kuwa klabu ya Simba inawalipa madeni watuhumiwa hao kiasi cha dola za Kimarekani 300,000 (Zaidi ya shilingi milioni 700 za kitanzania).
    Makosa mengine ni Aveva kutoa nyaraka za uongo kwa Benki ya CRDB Tawi la Azikiwe Dar es Salaam Machi 10, 2016, la tatu ni kutakatisha fedha kinyume cha sheria, ambapo inadaiwa rais huyo na Kaburu walikula njama za kufanya uhalifu huo.
    Shitaka la nne ni Kaburu kutakatisha fedha dola 300,000 na kuziweka katika Benki ya  Barclays Tawi la Mikocheni mjini Dar es Salaam, na la tano ni kutakatisha fedha  likimhusu tena, Makamu wa Rais, Kaburu anayedaiwa kumsadia Aveva kutakatisha fedha katika benki ya Barclays baada ya kughushi nyaraka.
    Kwa sasa nafasi zao zinakaimiwa na Salim Abdallah ‘Try Again’ katika Urais na Iddi Kajuna katika Makamu wa Rais, ambao wamejitahidi kuiongoza vizuri klabu tangu wenzao wapate matatizo hayo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KESI YA AVEVA, KABURU YAPIGWA KALENDA TENA, WARUDISHWA RUMANDE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top