• HABARI MPYA

    Tuesday, August 29, 2017

    MBAO FC YAPATA UDHAMINI MWINGINE, GF TRUCKS WAMWAGA MILIONI 70 NA BASI ‘KALI’

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KLABU ya Mbao FC ya Mwanza iliyo katika msimu wake wa pili tangu ipande Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, leo imeingia mkataba wa udhamini wa mwaka mmoja na kampuni ya uagizaji wa magari ya mizigo GF Trucks & Equpments wenye thamani ya Sh. Milioni 140.
    Akizungumza na Waandishi wa Habari kwenye ukumbi wa mikutano wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Ofisa Masoko wa kampuni hiyo, Kulwa Bundala amesema kwamba ndani ya mkataba huo wataipatia klabu hiyo basi lenye  thamani ya Sh. Milioni 70 pamoja na fedha taslimu Sh. Milioni 70.
    “Tumeingia mkataba wa mwaka mmoja na klabu hii kwa sababu tumeona jitihada zao katika mchezo huo, hivyo tunasaini nao mkataba  wenye thamani ya shilingi Milioni 140 na ndani ya mkataba huo tunawapatia basi lenye thamani ya shilingi Milioni 70 na milioni 70 nyingine tutawakabidhi fedha taslimu. Pia tunawapongeza Mbao FC kwa mwanzo mzuri wa Ligi kwa kuwafunga Kagera Sugar,” amesema Bundala.
    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa klabu hiyo Solly Zephania Njashi ameishukuru  kampuni ya GF kwa kuingia nao mkataba huo na basi hilo litawasaidia katika safari mbalimbali kipindi hiki cha Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    “Tunawashukuru GF kwa kukubali kutudhamini, fedha hizi pamoja na basi vitatusaidia kwenye klabu yetu, hasa basi litatusaidia sana katika safari za mikoani ambazo tutaenda kucheza mechi za Ligi Kuu, amesema Njashi.
    Huo unakuwa udhamini wa pili kwa washindi hao wa pili wa Azam Sports Federation Cup, baada ya mwaka jana kupata udhamini wa Hawaii Products Supplies, watengenezaji wa maziwa ya Cowbell wenye thamani ya Sh. Milioni 50 kwa msimu
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MBAO FC YAPATA UDHAMINI MWINGINE, GF TRUCKS WAMWAGA MILIONI 70 NA BASI ‘KALI’ Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top