• HABARI MPYA

    Wednesday, July 19, 2017

    KESI YA MANJI YAAHIRISHWA HADI AGOSTI 4

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KESI inayomkabili Mwenyekiti wa zamani wa Yanga SC, Yussuf Manji na wenzake wanne, imeahirishwa hadi Agosti 4 kupisha upelelezi zaidi.
    Hata hivyo leo Manji ambaye ni mtuhumiwa namba moja hakufika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kwa maelezo kwamba anaumwa na wakili wake akasema amepelekwa Zahanati ndogo ya Gereza la Keko anapatiwa matibabu, lakini watuhumiwa wengine wamefika mahakamani hapo.
    Julai 5 mwaka huu mahakama hiyo ilifika katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete mjini Dar es Salaam na kumsomea mashtaka Manji na wenzake watatu baada ya mtuhumiwa huyo kushindwa kufika mahakamani kutokana na matatizo ya kiafya yaliyosababishwa kulazwa hospitali.
    Kesi inayomkabili Mwenyekiti wa zamani wa Yanga SC, Yussuf Manji (katikati) na wenzake wanne imeahirishwa hadi Agosti 4 kupisha upelelezi zaidi

    Manji na wenzake watatu wamesomewa mashitaka saba wakidaiwa kutenda makosa mbalimbali katika nyakati tofauti jijini Dar es salaam.
    Mashtaka yanayowakabili watuhumiwa wote wanne ni pamoja na kujipatia bidhaa isivyo halali ambapo washtakiwa wote Juni 30 katika eneo la Chang'ombe Wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam askari polisi waliwakuta watuhumiwa wakiwa na majora 35 ya vitambaa vya kutengeneza sare za Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) zenye thamani ya shilingi milioni 192.5 isivyo halali.
    Katika shtaka jingine watuhumiwa wote wanatuhumiwa kukutwa na majora nane ya vitambaa vya kutengeneza sare za Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) vyenye thamani ya shilingi milioni 44 kinyume na sheria katika maeneo hayo ya Changombe huku katika shtaka jingine wakidaiwa kukutwa na mihuri ya JWTZ kinyume cha sheria.
    Pia wanatuhumiwa hao wanadaiwa kukutwa na mali inayodhaniwa kuwa imepatikana isivyo halali ambapo Julai mosi mwaka huu maeneo ya Chang'ombe A, walikutwa na namba za magari yenye usajili wa SU 383 inayodaiwa kupatikana isivyo halali.
    Watuhumiwa hao walisomewa mashtaka hayo mbele ya Hakimu mkazi mkuu wa mahakama hiyo, Haruma Shaidi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KESI YA MANJI YAAHIRISHWA HADI AGOSTI 4 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top