• HABARI MPYA

    Saturday, June 02, 2018

    NI MTIBWA SUGAR, AU SINGIDA UNITED KUBEBA KOMBE LA TFF LEO?

    Na Mahmoud Zubeiry, ARUSHA
    BINGWA mpya wa Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), au Azam Sports Federation Cup (ASFC) anatarajiwa kupatikana leo kwa mchezo wa fainali kati ya Singida United ya Singida na Mtibwa Sugar ya Morogoro vijijini.
    Mchezo huo unafanyika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mjini Arusha kuanzia Saa 10:00 jioni na utaonyeshwa moja kwa moja na Talevisheni ya Azam katika chaneli ya Azam Sports Two.
    Mtibwa iliingia fainali baada ya kuitoa Stand United kwa kuichapa 2-0, mabao yote akifunga Hassan Dilunga Uwanja wa CCM Kambarage mjini Shinyanga, wakati Singida United JKT Tanzania kwa kuichapa mabao 2-1 Uwanja wa Namfua mjini Singida.

    Na katika safari zao za msimu wa michuano hii timu zote hizo ziliving’oa vigogo, Mtibwa Sugar ikiwatoa Azam FC katika na SIngida United ikiwatupa Yanga, wote wakishinda kwa matuta baada ya sare ndani ya dakika 90.
    Hii itakuwa mechi ya nne ya msimu kuzikutanisha timu hizo baada ya kukutana kwenye Ligi Kuu mara mbili, moja wakitoa sare Morogoro na nyingine Mtibwa Sugar akishinda 3-0 Singida.   
    Lakini kwa sababu huu ni mchezo wa fainali, timu zote zinatarajiwa kuja na maarifa mapya, zaidi kucheza kwa tahadhari kubwa kuepuka kuruhusu mabao ya mapema.
    Singida United inayofundishwa na kocha Mholanzi, Hans van der Pluijm inajivunia nyota wake kama kiungo Tafadzwa Kutinyu, Kambale Salita, Deus Kaseke na wakongwe Nizar Kfalfan na Kiggi Makassy, wakati Mtibwa Sugar inajivunia wakali wake kama Dilunga, Stahmili Mbonde, Mohammed Issa ‘Banka’ na wakongwe Shaaban Mussa Nditi na Hussein Javu.  
    Katika fainali tatu za mashindano haya tangu yarejee rasmi, Yanga SC walikuwa wa kwanza kubeba taji mwaka juzi wakiifunga 3-0 Azam FC Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na Simba SC wakafuatia mwaka jana walipoifunga Mbao FC 2-1 Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.
    Ni Mtibwa Sugar au Mbao FC kubeba taji la ASFC leo Arusha? Bila shaka hilo ni jambo la kusubiri na kuona.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NI MTIBWA SUGAR, AU SINGIDA UNITED KUBEBA KOMBE LA TFF LEO? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top