• HABARI MPYA

    Monday, June 18, 2018

    DIAMOND KUFANYA ZIARA YA MAONYESHO KIBAO KARIBU MAREKANI YOTE

    Na Mahmoud Zubeiry, MARYLAND
    MWANAMUZIKI Nassib Abdul Juma maarufu kwa jina la sanaa kama Diamond Platnumz, anatarajiwa kuwa na ziara kubwa na ndefu nchini Marekani ya kutumbuiza katika majimbo tofauti kati ya Juni na Julai, mwaka huu.
    Ziara hiyo ya Diamond mwenye umri wa miaka 28, itajulikana kama 'Diamond Platinumz A Boy From Tandale USA Tour 2018' na tayari Watanzania waishio sehemu mbalimbali nchini Marekani wanajipanga kwa maonyesho yake kwenda kumsapoti ndugu yao.
    Matangazo ya ziara za Diamond Platinumz yamekwishaanza hapa Marekani na onyesho lake la kwanza litafanyika Oakland, California Juni 22 kabla ya kwenda kutumbuza Los Angeles Juni 23, Kansas City Juni 29 na Columbus Ohio Juni 30, mwaka huu.

    Diamond Platnumz, anatarajiwa kutumbuiza katika majimbo tofauti Marekani kati ya Juni na Julai, mwaka huu

    Baba huyo wa watoto watatu, Princess Latifa, Prince Nylan aliozaa na Mganda Zarina Hassan maarufu Zari the Boss Lady na Dylan aliyezaaa na binti wa nyumbani, Hamisa Mobetto atatumbuiza pia Washington DC Julai 3, New York City Julai 4, Chicago Julai 6, Twin Cities Minnesota Julai 7, Atlanta Julai 13, Boston Julai 14, Dallas Texas Julai 20 na Houston Julai 21, mwaka huu.  
    Diamond ni mwanamuziki mkubwa kwa sasa Afrika ambaye ana mashabiki sehemu mbalimbali duniani na kwa hapa Marekani anapendwa zaidi na watu wa Nigeria na Afrika Mashariki, nchi za Kenya, Uganda na Tanzania anakotokea na maonyesho yake yanatarajiwa kuvutia watu wa huko zaidi.
    Akiwa anatamba na nyimbo zake nzuri kama Iyena Iyena aliyotoa hivi karibuni akimshirikisha mtoto wa nyumbani kutola lebo ya WCB, Rayvany, African Beauty alioimba na Omarion, Mary You alioimba na Ne-Yo wote wa Marekani, Number One aliomshirikisha msanii kutoka Nigeria, Davido na nyinginezo - Diamond anatarajiwa kukonga nyoyo za mashabiki wake wa hapa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: DIAMOND KUFANYA ZIARA YA MAONYESHO KIBAO KARIBU MAREKANI YOTE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top