• HABARI MPYA

    Tuesday, June 26, 2018

    SIMBA SC YAMSAINISHA MIAKA MIWILI MEDDIE KAGERE…SERGE WAWA MAZUNGUMZO YANAENDELEA

    Na Esther Marwa, DAR ESSALAAM
    KLABU ya Simba SC ya Dar es Salaam imeimarisha kikosi chake kuelekea michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, maarufu kama Kombe la Kagame baada ya kumsajili mshambuliaji Meddie Kagere kutoka Gor Mahia ya Kenya.
    Kagere, Mnyarwanda mwenye asili ya Uganda leo amesaini mkataba wa miaka miwili mbele ya Rais wa Simba, Salim Abdallah ‘Try Again’ mjini Dar es Salaam na mara moja atajiunga na wachezaji wenzake wapya kwa mazoezi ya kujiandaa na Kombe la Kagame, michuano itakayoanza Juni 29 nchini Tanzania.
    Kagere mwenye umri wa miaka 31, mchezaji wa zamani wa kimataifa wa Rwanda, amekuwa mshambuliaji tegemeo wa Gor Mahia kwa miaka minne iliyopita tangu ajiunge nayo akitokea KF Tirana ya Albania iliyokuwa Ligi Kuu ambako alicheza kwa mwaka mmoja tu akitokea Rayon Sports ya Kigali iliyomuuza kwa dola za Kimarekani 10,000.

    Meddie Kagere (kushoto) akisaini mkataba wa miaka miwili kujiunga na Simba SC akitokea Gor Mahia ya Kenya 

    Kagere, Mnyarwanda mwenye asili ya Uganda leo amesaini mkataba wa miaka miwili mbele ya Rais wa Simba, Salim Kagere, mzaliwa wa Kampala aliyeichezea Amavubi mechi 30 tangu mwaka 2011 na kuifungia mabao 10, kisoka aliibukia Mbale Heroes ya Uganda mwaka 2004 ambako alicheza hadi mwaka 2006 alipohamia ATRACO FC ya Rwanda.
    Mwaka 2007 alihamia Kiyovu Sports alikocheza hadi 2008 alipohamia Mukura Victory hadi 2010 alipojiunga na Polisi FC alikocheza hadi 2012 alipohamia Zarzis ya Tunisia ambako alidumua kwa mwaka mmoja tu. Alirudi Polisi ya Rwanda mwaka 2013 na kucheza hadi 2014 alipohamia Rayon Sports.
    Na baada ya kucheza KF Tirana na Gor Mahia kufuatia kuondoka Rwanda, Kagere anahamishia maisha yake ya soka nchini Tanzania.
    Kutua kwa Kagera Simba SC ni pigo kwa mahasimu wao wa jadi, Yanga ambayo nao walikuwa wanamuwania kwa sera za Mwenyekiti wa Kamati ya Usimamizi wa klabu kwa sasa, Tarimba Abbas ‘Kimya Kimya’ .
    Lakini upande wa pili, Yanga inayoshiriki Kombe la Shirikisho Afrika ikiwa Kundi D imepata ahueni, kwani wapinzani wao Gor Mahia wamepunguziwa nguvu kwa kumpoteza tegemeo lake la mabao kuelekea mchezo ujao, Julai 18 Uwanja wa Moi Kasarani nchini Kenya. 
    Katika hatua nyingine, beki wa zamani wa El Merreikh ya Sudan na Azam FC ya Dar es Salaam, Muivory Coast, Serge Wawa Pascal yupo mazoezini na Simba SC huku mazungumzo ya kusajiliwa yakiendelea chini ya Mwenyekiti, Salim. Wawa naye alikuwa anatajwa kuwa mbioni kutua Yanga.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC YAMSAINISHA MIAKA MIWILI MEDDIE KAGERE…SERGE WAWA MAZUNGUMZO YANAENDELEA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top