• HABARI MPYA

    Friday, June 01, 2018

    BANDA NA UHURU HAWANA MAPUMZIKO, WAENDELEA KUJIFUA KATIKA LIKIZO

    Na Rehema Lucas, DAR ES SALAM
    PAMOJA na kwamba wapo nchini kwa mapumziko ya baada ya msimu, wachezaji wawili wa Tanzania wanaocheza Afrika Kusini, beki Abdi Hassan Banda na kiungo Uhuru Suleiman Mwambungu wanaendelea na mazoezi. 
    Nyota hao waliowahi kucheza kwa wakati tofauti klabu za Coastal Union na Simba SC, wapo kwa mapumziko kisiwani Zanzibar, lakini huko pia wameendelea kufanya mazoezi.
    Banda anayechezea Baroka FC ya Ligi Kuu ya ABSA Afrika Kusini na Uhuru wa Mthatha Bucks FC ya Daraja la Kwanza wote wameposti picha wakiwa ufukweni mwa Bahari ya Hindi kisiwani Zanzibar wakifanya mazoezi kujiweka fiti japo wapo mapumzikoni.
    Abdi Banda ameendelea na mazoezi japo yupo nchini kwa mapumziko ya baada ya msimu


    Uhuru Suleiman (kushoto) akiwa na Abdi Banda na rafiki zao baada ya mazoezi 

    Hata hivyo, Banda mume mtarajiwa wa Zabib Kiba, dada wa mwanamuziki Ali Kiba hakuwa na msimu mzuri sana wa kwanza Baroka FC, kwani timu hiyo ilinusurika kushuka daraja.
    Banda ataendelea kucheza Ligi Kuu ya ABSA Afrika Kusini msimu ujao pamoja na timu yake, Baroka FC kuchapwa bao 1-0 na SuperSport United katika mchezo wa mwisho wa ligi hiyo Uwanja wa Lucas Masterpieces Moripe mjini Pretoria mwezi uliopita.
    Baroka imekuwa timu ya mwisho baada ya timu mbili, Platinum Stars na Ajax Cape Town kuteremka, ikiwa imejikusanyia pointi 34 katika mechi 30.
    Kwa upange wake, Uhuru ambaye alimtangulia Banda kote Coastal Union na Simba SC timu yake imesajili Daraja la Kwanza kwa mwaka wa tatu tangu ipande 2015.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BANDA NA UHURU HAWANA MAPUMZIKO, WAENDELEA KUJIFUA KATIKA LIKIZO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top