• HABARI MPYA

    Sunday, July 02, 2017

    UCHAGUZI TFF WASITISHWA BAADA YA KAMATI KUTOFAUTIANA KUHUSU MALINZI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MCHAKATO wa Uchaguzi Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) umesitishwa kwa muda hadi hapo itakapotangazwa tena baadaye.
    Hatua hiyo imetangazwa leo na Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi, Wakili Rovocatus Kuuli katika mkutano na Waandishi wa Habari ofisi za TFF, Uwanja wa Kaarume, Dar es Salaam na baadaye kuthibitishwa na Kaimu Katibu Mkuu wa shirikisho, Salum Madadi.
    Wakili Kuuli amesema baada ya kutofautiana na Wajumbe wenzake jana kuhusu wagombea ambao wanashikiliwa na vyombo dola kupitishwa moja kwa moja kwenye uchaguzi baada ya kukosekana kwenye usaili, wamekubaliana kwanza kusitisha mchakato huo.


    Rais wa TFF, Jamal Malinzi (kushoto) na Katibu wake, Selestine Mwesigwa (katikati) wako rumande baada ya kunyimwa dhamana Alhamisi na anatarajiwa kufikishwa tena Mahakamani kesho



    Na lengo ni kujaribu kutafuta suluhu ya tofauti hizo kabla ya kufikia makubaliano ili mchakato uendelee. Na Msemaji wa TFF, Alfred Lucas akafafanua kwamba uchaguzi wa TFF upo kama ulivyopangwa, isipokuwa mchakato ndiyo umesimama kwa muda kutafuta suluhu ya masuala kadhaa. 
    Na hatua hiyo inachukuliwa siku moja baada ya Kamati ya Utendaji ya TFF iliyokutana jana Dar es Salaam kumpitisha Wallace Karia kuwa Kaimu Rais wa shirikisho hilo na Mkurugenzi wa Ufundi wa TFF, Salum Madadi kuwa Kaimu Katibu Mkuu hadi hapo mahakama itakapoamua kuhusu kesi zinazowakabili kwa sasa Rais, Jamal Malinzi na Katibu Mkuu, Mwesigwa Selestine. 
    Malinzi, Mwesigwa kwa pamoja na Mhasibu wa TFF, Nsiande Isawafo Mwanga wako rumande baada ya kunyimwa dhamana Alhamisi na wanatarajiwa kufikishwa tena Mahakamani Jumatatu.
    Watatu hao, Alhamisi walisomewa mashitaka 28 ya kughushi na kutakatisha fedha kupitia akaunti ya TFF iliyopo katika banki ya Stanbic, Dar es Salaam.
    Hakimu mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Kisutu, Dar es Salaam, Wilbord Mashauri aliwanyima dhamana watatu hao kufuatia mabishano ya kisheria baina ya mawakili wa utetezi dhidi ya mawakili wa upande wa Serikali.                        
    Na Ujumbe wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA) unatarajiwa kuwasili nchini kesho kuja kufuatilia sakata zima la viongozi hao wa TFF kufikishwa kwenye vyombo vya dola na kwa ujumla hali halisi ndani ya shirikisho.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: UCHAGUZI TFF WASITISHWA BAADA YA KAMATI KUTOFAUTIANA KUHUSU MALINZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top