• HABARI MPYA

    Saturday, July 22, 2017

    STARS SARE 0-0 NA RWANDA KIGALI, YATUPWA NJE CHAN 2019

    Na Innocent Okama, KIGALI
    TANZANIA imeondolewa mapema kwenye michuano ya Ubingwa wa Mataifa ya Afrika (CHAN), inayoshirikisha wachezaji wanaocheza nchini mwao pekee, baada ya kulazimishwa sare ya 0-0 na wenyeji Rwanda Uwanja wa Kigali, uliopo Nyamirambo mjini Kigali leo.
    Matokeo hayo yanamaanisha Taifa Stars inaondolewa kwa bao la ugenini, kufuatia kulazimishwa sare ya 1-1 kwenye mchezo wa kwanza Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza Jumamosi iliyopita.
    Rwanda leo walicheza mchezo wa kujihami kulinda matokeo ya ugenini, muda mwingi wakiwa katika eneo lao kujilinda na kushambulia kwa kushitukiza.

    Kiungo mkongwe wa Tanzania, Erasto Nyoni (kulia) akipambana na mchezaji wa Rwanda Uwanja wa Nyamirambo 

    Na kwa mara nyingine, Taifa Stars ya kocha Salum Shaaban Mayanga imeonyesha ubutu wake katika safu ya ushambuliaji baada ya kupoteza nafasi nyingi za wazi.
    Mshambuliaji mkongwe John Raphael Bocco atalala na mawazo leo, kwani peke yake alipoteza nafasi tatu nzuri za kufunga mabao, tena zile za kumalizia tu baada ya kupelekewa pasi nzuri za uhakika.
    Lakini kwa ujumla wachezaji wote wa mbele, Shiza Ramadhani Kichuya, Simon Happygod Msuva na Bocco walikosa mipango ya kuingiza mpira kwenye nyavu za Rwanda waliokuwa na mchezo mwingine mwepesi leo.   
    Marefa wa Uganda, Brian Nsubuga Miro aliyepuliza filimbi akisaidiwa na Ronald Katenya na Dick Okello walichezesha kwa haki leo. Kwa matokeo hayo, Rwanda itakutana na Uganda, iliyoitoa Sudan Kusini katika hatua ya mwisho ya mchujo kuwanian tiketi ya CHAN ya mwakani nchini Kenya.
    Kwa kocha Mayanga, huu unakuwa mchezo wa tatu mfululizo wa mashindano ya yanayotambuliwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kucheza bila ushindi zote akitoa sare, ukiwemo ule wa sare ya 1-1 na Lesotho Dar es Salaam kufuzu AFCON ya Cameroon 2019.
    Kikosi cha Rwanda kilikuwa; Ndayishimiye Eric, Rucogoza Aimable, Nsabimana Aimable, Yanick mukunzi, Kevin Muhire/Latif Bishira dk67, Mico Justin, Thierry Manzi, Eric Iradukunda, Emmanuel Imanishimwe, Dominique Savio Nshuti/Kayumba Soter dk 91 na Djihad Bizimana.
    Tanzania; Aishi Manula, Boniphace Maganga, Gardiel Michael, Erasto Nyoni, Salim Mbonde, Himid Mao, Simon Msuva/Joseph Mahundi dk66, Muzamil Yassin, John Bocco ‘Adebayor’, Raphael Daudi/Said Ndemla dk 62 na Shiza Kichuya.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: STARS SARE 0-0 NA RWANDA KIGALI, YATUPWA NJE CHAN 2019 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top