• HABARI MPYA

    Monday, July 17, 2017

    KESI YA MALINZI YAAHIRISHWA TENA HADI JULAI 31

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KESI inayowakabili viongozi wakuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Rais Jamal Malinzi na Katibu weke, Selestine Mwesigwa imeahirishwa tena hadi Julai 31, ili kupisha upepelezi zaidi.
    Mapema hii leo, wawili hao pamoja na Mkurugezi wa Fedha wa TFF, Isinde Isawafo Mwanga walifikishwa tena mahakama ya Hakimu Mkazi, Kisutu mjini Dar es Salaam, hiyo ikiwa ni mara ya tatu na kusomewa mashitaka yao 28, kabla ya kesi hiyo kupelekwa tena mbele hadi Julai 31.
    Hakimu mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Wilbroad Mashauri, alisema anaiahirisha kesi hiyo tena kwa sababu upelelezi haujakamilika wa washtakiwa wanarudi rumande hadi Julai 31 kesi hiyo itakapotajwa tena.
    Malinzi, pamoja na Katibu wa TFF, Selestine Mwesigwa na Mhasibu, Nsiande Isawafo Mwanga walipelekwa rumande Juni 29 baada ya kusomewa mashitaka 28 ya kughushi na kutakatisha fedha kupitia akaunti ya TFF iliyopo katika banki ya Stanbic, Dar es Salaam.
    Walirudishwa Mahakamani Julai 3, ambako walinyimwa dhamana tena na kurejeshwa rumande hadi leo, Julai 17 kwa sababu za upepelezi kutokamilika.
    Katika mashitaka hayo, 25 yanakwenda moja kwa moja kwa Rais wa shirikisho hilo, Malinzi akidaiwa kughushi michakato mbalimbali ya kifedha, huku matatu yakiwahusu wote na Katibu wake na Mhasibu wake Nsiande Isawafo Mwanga.
    Malinzi aliingia madarakani TFF Oktoba mwaka 2013 baada ya kupata kura 72 kati ya 126 zilizopigwa akimshinda aliyekuwa mpinzani wake wa karibu, Athumani Nyamlani.
    Lakini baada ya kesi hii kuanza kuunguurma na kuwekwa rumande, Kamati ya Utendaji ya TFF ilikutana na kumteua Makamu wake, Wallace Karia kukaimu Urais wa shirikisho hilo.
    Lakini kwa mwenendo wa kesi, Malinzi ndiyo kama amekwishaaga TFF, kwani uchaguzi unatarajiwa kufanyika Agosti 12 mjini Dodoma naye hajashiriki usaili wa wagombea, hivyo haruhusiwi tena kugombea.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KESI YA MALINZI YAAHIRISHWA TENA HADI JULAI 31 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top