• HABARI MPYA

    Friday, July 21, 2017

    KASEKE KWAHERI YANGA, AKUBALI KUTUA SINGIDA UNITED

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    KOCHA Mholanzi, Hans van der Pluijm ameendelea kuiumiza timu yake ya zamani, Yanga SC baada ya leo kufikia makubaliano na kiungo Deus David Kaseke.
    Akizungumza na Bin Zubeiry Sports – Online leo mjini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Singida United, Sanga Festo amethibitisha mpango wa kumchukua mchezaji huyo mwenye nguvu na uwezo mkubwa wa kumiliki mpira.
    “Kweli tumekwishafikia makubaliano naye (Kaseke), hivyo kesho ataungana na wenzake Mwanza kwa ajili ya maandalizi ya msimu mpya,” amesema Sanga Festo.
    Kiungo Deus Kaseke amekubali kuondoka Yanga akajiunge na Singida United

    Kaseke ambaye Agosti 27, mwaka huu atatimiza umri wa miaka 23, anakuwa mchezaji wa pili wa Yanga ndani ya wiki moja kuhamia Singida United, baada ya mwanzoni mwa wiki kipa Ally Mustafa ‘Barthez’ kutangulia.
    Na wote wanaondoka Jangwani kama wachezaji huru baada ya kumaliza mikataba yao na klabu hiyo bingwa ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Kaseke alijiunga na Yanga mwaka juzi akitokea Mbeya City ya Mbeya na baada ya miaka miwili ya kushinda mataji mawili ya Ligi Kuu, Ngao ya Jamii na Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), au Azam Sports Federation Cup (ASFC) kwake imtosha na anakwenda kutafuta changamoto nyingine.
    Dalili za Kaseke kuondoka Yanga zilianza kuonekana mapema tu, kutokana na kuchukua muda mrefu katika majadiliano ya mkataba mpya. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KASEKE KWAHERI YANGA, AKUBALI KUTUA SINGIDA UNITED Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top