• HABARI MPYA

    Wednesday, November 20, 2019

    MWINA KADUGUDA ATEULIWA KUKAIMU UENYEKITI SIMBA SC, SALUM ‘TRY AGAIN’ MAKAMU WAKE

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MJUMBE wa Bodi ya Wakurungenzi ya Klabu ya Simba Mwina Kaduguda ameteuliwa kuwa Kaimu Mwenyekiti wa klabu hiyo, nafasi iliyoachwa wazi na Swedy Mkwabi ambaye alijiuzulu Septemba 19 mwaka huu.
    Taarifa iliyotolewa leo na Mtendaji Mkuu wa klabu hiyo Senzo Mbatha imeeleza kuwa uteuzi huo uliofanywa na bodi ya wakurugenzi umeanza Novemba 19, 2019 na tarahe ya uchaguzi wa kujaza nafasi hiyo itatangazwa hivi karibuni.
    Katika hatua nyingine, Salum Abdallah Muhene ‘Try Again’ kuwa Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Kampuni ya Simba SC Limited kuanzia Novemba 19, 2019.
    Mkwabi alijiuzulu wadhifa huo miezi 10 na ushei tu tangu achaguliwe, akisema kwamba ameamua kujiuzulu kwa sababu mambo si shwari ndani ya klabu na wakati ukifika kila kitu kitakuwa bayana.

    Lakini taarifa ya klabu hiyo siku hiyo ilisema kwamba Mkwabi aliiandikia Bodi ya Wakurugenzi kupitia Mwenyekiti wa Bodi, Mohammed ‘Mo’ Dewji akisema sababu kuu ya kijiuzulu nafasi hiyo ni kuhitaji muda zaidi kusimamia shughuli zake binafsi.
    Nkwabi alipita bila kupingwa Novemba 5, mwaka 2018 katika uchaguzi uliofanyika ukumbi wa mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere mjini Dar es Salaam, akiwa mgombea pekee baada ya gwiji wa klabu, Mtemi Ramadhani kujitoa dakika za mwishoni.
    Katika nafasi za Ujumbe waliochaguliwa ni Hussein Kitta Mlinga, Dk. Zawadi Ally Kadunda, Suleiman Haroub Said, Mwina Mohammed Kaduguda na Asha Ramadhani Baraka.
    Uchaguzi wa Simba SC ulifuatia uongozi uliopita ulioingia madarakani Juni 30, mwaka 2014 chini ya Rais, Evans Elieza Aveva, Makamu wa Rais, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ na Wajumbe Iddi Kajuna, Said Tully, Collins Frisch, Ally Suru na Jasmine Badour kumaliza muda wake.
    Lakini Aveva na Kaburu hawakufanikiwa kumalizia muda wao madarakani, kufuatia kuwekwa rumande katika gereza la Keko tangu Juni 29, mwaka 2017 kwa tuhuma za kughushi nyaraka, kesi ambayo bado inaendelea katika Mahakama ya Kisutu mjini Dar es Salaam.
    Na Julai 1, mwaka huo, Kamati ya Utendaji iliwateua Salum Abdallah ‘Try Again’ na Iddi Kajuna kukaimu nafasi za Aveva na Kaburu na hao ndiyo waliosimamia mchakato mzima wa mabadiliko ya klabu kuelekea uchaguzi uliomuweka madarakani Mkwabi na wenzake.
    Lakini taarifa za ndani za klabu zinasema Mkwabi hakuwa na maelewano mazuri na Mwenyekiti wa Bodi ya klabu, mfanyabiashara Mohamed ‘Mo’ Dewji, Mbunge wa zamani wa Singida Mjini ambaye ameshinda zabuni ya kununua asilimia 49 za hisa za klabu ya Simba SC.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MWINA KADUGUDA ATEULIWA KUKAIMU UENYEKITI SIMBA SC, SALUM ‘TRY AGAIN’ MAKAMU WAKE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top