• HABARI MPYA

    Thursday, August 03, 2017

    MSIMU MPYA WA LIGI KUU YA VODACOM WAZINDULIWA LEO DAR

    Na Rehema Lucas, DAR ES SALAAM
    MSIMU mpya wa Ligi Kuu ya soka ya Vodacom Tanzania Bara umezinduliwa rasmi leo kwa wadhamini wakuu, kampuni ya Vodacom Tanzania kukabidhi vifaa kwa timu zote 16 zitakazoshiriki ligi hiyo msimu ujao.
    Zoezi hilo limefanyika mjini Dar es Salaam leo na Vodacom wanaodhamini Ligi Kuu inayorushwa moja kwa moja na Azam TV, wamekabidhi vifaa mbalimbali zikiwemo jezi, viatu, mipira na suti za kimichezo.
    Akikabidhi vifaa hivyo, Mkurugenzi wa Idara ya Masoko ya Vodacom, Hisham Hendi amesema kwamba, kwa mara nyingine tena katika kuhakikisha Ligi Kuu ya soka hapa nchini inaenda vizuri wanakabidhi vifaa vya ubora wa hali ya juu.
    Msemaji wa Simba SC, Hajji Sunday Manara (katikati) akisalimiana na vijana waliokuwa wanaonyesha jezi za Yanga katika uzinduzi huo
    Hajji Manara akiwa katikati ya vijana walioonyesha jezi za Simba
    Viongozi wa Vodacom, Bodi ya Ligi na klabu zote 16 za Ligi Kuu wakiwa katika picha ya pamoja

    Hendi amesema kwamba pia Vodacom imefurahishwa na klabu zilizopanda Ligi Kuu msimu huu kutoka Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara, Singida United, Lipuli na Mji Njiombe FC kuwa zimejiandaa vizuri kwa ushindani.
    “Tunajisikia furaha kukabidhi vifaa hivi tukiwa tunatakeleza matakwa ya mkataba wa udhamini  na ni imani yetu kwamba timu zitakazoshiriki Ligi Kuu zimejiandaa vya kutosha kwa msimu mpya wa Ligi,” amesema Hendi
    Kwa upande wake, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi, Boniphace Wambura ameishukuru  Vodacom Tanzania na kuzitaka klabu zinazoshiriki Ligi Kuu kuzingatia na kuheshimu nembo ya mdhamini wakati wa mechi.
    Wambura amesema Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) halipendi kutumia kanuni na sheria kuziadhibu klabu zitazokwenda kinyume na maelekezo hayo.
    Ameongeza kwamba, msimu huu wa Ligi Kuu utakuwa bora kutokana na maandalizi yote kukamilika mapema – pia timu zitakazoshiriki kuwa zimejiandaa vizuri.
    Timu nyingine zinazoshiriki Ligi Kuu ni mabingwa, Yanga SC, washindi wa pili, Simba SC, wa tatu, Kagera Sugar, wa nne Azam FC, wa tano Mtibwa Sugar, wa sita Stand United, wa saba Ruvu Shooting, wa nane Tanzania Prisons, wa tisa Maji Maji, wa 10 Mwadui, wa 11 Mbeya City, wa 12 Mbao FC na wa 13 Ndanda FC.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MSIMU MPYA WA LIGI KUU YA VODACOM WAZINDULIWA LEO DAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top