• HABARI MPYA

    Sunday, August 21, 2016

    SAMATTA APIGA MBILI GENK IKIUA 3-0 UGENINI LIGI YA UBELGIJI

    Na Mwandishi Wetu, LOKEREN
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta amefunga mabao mawili timu yake, KRC Genk ya Ubelgiji ikishinda 3-0 dhidi ya wenyeji, Lokeren Uwanja wa Daknamstadion mjini Lokeren katika mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji.
    Samatta alifunga mabao yote mawili ya mwanzo, la kwanza dakika ya 34 na la pili dakika ya 38, yote akisetiwa na kiungo kutoka Hispania, Alejandro Pozuelo Melero aliyemsetia pia Mjamaica Leon Bailey kufunga la tatu dakika ya 48.
    Baada ya ushindi huo katika hatua ya awali ya Ligi ya Ubelgiji, Samatta anatarajiwa kuiongoza tena Genk Alhamisi katika mchezo wa marudiano hatua ya mwisho ya mchujo wa kuwania kuingia hatua ya makundi ya Europa League dhidi ya Lokomotiva Zagreb ya Croatia.
    Samatta (kulia) akipongezwa na wenzake jana baada ya kufunga
    Genk watakuwa nyumbani Alhamisi Uwanja wa Luminus Arena, baada ya kulazimisha sare ya 2-2 katika mchezo wa kwanza Uwanja wa Maksimir mjini Zagreb.
    Samtta alifunga pia bao la pili la Genk katika sare ya 2-2 na Lokomotiva Zagreb dakika ya 47, baada ya Leon Bailey kutangulia kuifungia timu hiyo kwa penalti dakika ya 36.
    Mabao ya wenyeji yalifungwa na Mirko Maric kwa penalti dakika ya 52 na Ivan Fiolic dakika ya 59.
    Genk sasa itahitaji sare ya bila mabao au ushindi mwembamba hata wa 1-0 katika mchezo wa marudiano Alhamisi ijayo ili kufuzu makundi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA APIGA MBILI GENK IKIUA 3-0 UGENINI LIGI YA UBELGIJI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top