• HABARI MPYA

    Sunday, March 13, 2016

    ULIMWENGU AFANYA MAMBO, MAZEMBE YALAZIMISHWA SARE 2-2 LIGI YA MABINGWA

    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Thomas Ulimwengu (pichani kushoto) amehusika katika mabao yote mawili ya TP Mazembe ikilazimishwa sare ya 2-2 na wenyeji St George katika mchezo wa kwanza wa Raundi ya Kwanza Ligi ya Mabingwa Afrika leo nchini Ethiopia. 
    Katika mchezo huo uliofanyika Uwanja wa Bahir Dar nje kidogo ya mji wa Addis Ababa, Ulimwengu alicheza kwa dakika 63 kabla ya kumpisha Rogger Asale.
    Akicheza mechi yake ya kwanza baada ya kupona maumivu ya mguu yaliyomuweka nje tangu Januari, Uliwengu alimsetia Daniel Adjei kuifungia bao la kwanza Mazembe dakika ya pili ya muda wa nyongeza baada ya dakika 45 za kipindi cha kwanza kutimia.
    Na Ulimwengu tena akapiga mpira uliombabatiza mchezaji wa St George, Isaac Isiende na kutinga nyavuni kuipatia Mazembe bao la pili dakika ya 46, yaani mwanzoni tu mwa kipindi cha pili.
    Mabao ya St George yamefungwa na Assefa Behailu dakika ya 11 na Girma Adane dakika ya 60 na sasa Mazembe, mabingwa watetezi wa michuano hiyo wanaweza kusonga mbele hata kwa sare ya 0-0 nyumbani Lubumbashi wiki ijayo.
    Kikosi cha Mazembe kilikuwa; Gbohouo, Kabaso, Kimwaki, Coulibaly, Kasusula, Bope, Kouame, Adjei, Ulimwengu/Assale dk63, Bolingi/Luyindama dk90 na Traore/Singuluma dk85.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ULIMWENGU AFANYA MAMBO, MAZEMBE YALAZIMISHWA SARE 2-2 LIGI YA MABINGWA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top