• HABARI MPYA

    Friday, March 25, 2016

    STARS YAWASILI ‘HOI BIN TAABAN’ DAR

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    KIKOSI cha timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, kimewasili Dar es Salaam usiku huu wachezaji wake wakiwa wamechoka baada ya safari ndefu tangu mchana kutoka D’jamena, Chad kupitia Addis Ababa, Ethiopia.
    Mara baada ya kuwasili, Taifa Stars walipokewa na Katibu wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Mohamed Kiganja ambaye aliwapa hotuba fupi ya mapokezi.
    Stars ambayo Jumatano iliwafunga wenyeji Chad 1-0 katika mchezo wa Kundi G kufuzu Kombe la Mataifa ya Afrika Uwanja wa Omnisports Idriss Mahamat Ouya mjini D’jamena mara baada ya kuwasili, ilikwenda moja kwa moja kambini, hoteli ya Urban Rose, katikati ya jiji.
    Nahodha Mbwana Samatta akiwaongoza wachezaji wake kutoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam baada ya kuwasili usiku huu

    Wachezaji waliowasili na Taifa Stars usiku huu kutoka Chad ni makipa; Aishi Manula na Ally Mustafa ‘Barthez’.
    Mabeki; Juma Abdul, Shomary Kapombe, Mwinyi Hajji, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Erasto Nyoni, Kevin Yondan na David Mwantika.
    Viungo; Jonas Mkude, Mwinyi Kazimoto, Himid Mao, Mohammed Ibrahim, Ibrahim Hajib, Deus Kaseke, Farid Mussa na Shiza Kichuya.
    Washambuliaji ni John Bocco, Thomas Ulimwengu na Nahodha Mbwana Samatta.
    Thomas Ulimwengu akitoka Uwanja wa Ndege baada ya kuwasili
    Katibu wa BMT, Mohammed Kiganja akiwahutubia wachezaji Uwanja wa Ndege
    Wachezaji wa Taifa Stars wakimsikiliza Katibu wa BMT
    Wachezaji wa Taifa Stars wakimsikiliza kwa makini Katibu wa BMT
    Baadhi ya viongozi na wachezaz wakitoka Uwanja wa Ndege baada ya kuwasli
    Kutoka kulia ni Jonas Mkude, Aishi Mnula na Shiza Kichuya wakiwa Uwanja wa Ndege wa Addis Ababa, Ethiopia wakisubiri kuunganisha ndege ya kuja Dar es Saalaam 

    Wachezaji hao wataungana na wachezaji wengine sita waliobaki kambini Dar es Salaam, ambao ni kipa Shaaban Kado, viungo Ismail Khamis ‘Suma’, Said Ndemla na washambuliaji Elias Maguri, Jeremiah Juma na Abdillah Yussuf ‘Adi’. 
    Stars inashika nafasi ya tatu katika Kundi G, ikiwa na pointi nne baada ya kushinda mechi moja dhidi ya Chad, kufungwa na Misri 3-0 na kutoa sare ya 0-0 na Nigeria.
    Misri inaongoza Kundi hilo kwa pointi zake sita, ikifuatiwa na Nigeria yenye pointi nne sawa na Tanzania, lakini ina wastani mzuri wa mabao, wakati Chad inashika mkia haina pointi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: STARS YAWASILI ‘HOI BIN TAABAN’ DAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top