• HABARI MPYA

    Monday, March 28, 2016

    MASHABIKI WAKINUKISHA KENYA IKIPIGWA 1-0 NYUMBANI AFCON

    POLISI nchini Kenya wamelazimika kuwalipulia mabomu ya machozi mashabiki Uwanja wa Nyayo, baada ya kuanzisha vurugu wakati timu yao ya taifa, Harambee Stars ikimenyana na Guinea Bissau.
    Vurugu hizo zilianza baada ya Guinea Bissau inayoshika nafasi ya 147 katika viwango vya ubora wa soka duniani kupata bao la utata lililowapa ushindi wao wa kwanza ugenini kihistoria katika mechi za mashindanio wakiilaza Kenya 1-0 na kupanda kileleni mwa Kundi E.
    Mshambuliaji mzaliwa wa Ureno, Cicero alifunga bao hilo la ushindi dakika ya 81 na kuzusha balaa uwanjani kiasi cha mchezo kusimama kwa zaidi ya dakika 30.


    Mshika kibendera alikubali bao hilo lililofungwa na Cicero kwa kichwa baada ya mpira wa kona, ambao licha ya kudakwa na kipa wa Kenya, Arnold Origi alisema ulikuwa umekwishavuka mstari wa lango.
    Hali hiyo iliamsha hasira za wachezaji wa Kenya na mashabiki wao na kuanza kufanya fujo, kiasi cha Polisi kwenda kuwadhibiti kwa mabomu ya machozi.
    Guinea Bissau sasa inafikisha pointi saba, wakiizidi pointi moja Kongo na mabingwa wa AFCON ya 2012, Zambia katika Kundi E.
    Mechi nyingine ya kundi hilo Jumapili, Kongo na Zambia zimetoka sare ya 1-1 mjini Brazzaville. Jordan Massengo, anayecheza timu ya daraja la chini Ufaransa alianza kuifungia Kondo dakika ya 48, kabla ya Winston Kalengo kuisawazishia Zambia dakika ya 70.
    Rekodi ya Ghana kushinda mfululizo mechi za kufuzu AFCON leo imezimwa baada ya kulazimishwa sare ya bila kufungana na Msumbiji mjini Maputo.
    Nahodha Stephane Sessegnon ameifungia mabao mawili Benin ikiichapa Sudan Kusini 4-1 na kuendeleza rekodi ya kutofungwa katika Kundi C wakizidi kupaa kileleni.
    Joel Mogorosi amefunga bao la ushindi mjini Francistown timu yake, Botswana ikiilaza 2-1 Comoros katika Kundi D.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MASHABIKI WAKINUKISHA KENYA IKIPIGWA 1-0 NYUMBANI AFCON Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top