• HABARI MPYA

    Sunday, March 13, 2016

    SIMBA SC SHEREHE…NI SHEREHE ZA USHINDI KUELEKEA UBINGWA, PRISONS AFA 1-0 TAIFA

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    BAO pekee la kiungo Awadh Juma Issa (pichani kushoto) limeizidi kuisogeza Simba SC jiani na ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kufuatia ushindi wa 1-0 dhidi ya Prisons jioni ya leo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Awadh alifunga bao hilo dakika ya 86 kwa shuti la mita 19 na ushei akimalizia pasi ya kiungo Jonas Gerald Mkude, baada ya kuingia kutokea benchi kuchukua nafasi ya kiungo Mzimbabwe, Justice Majabvi.
    Na Wekundu wa Msimbazi sasa wanafikisha pointi 54 baada ya kucheza mechi 23 wakiwazidi pointi nne, mabingwa watetezi, Yanga SC walio nafasi ya pili, lakini wamecheza mechi pungufu, 21. Azam FC yenye pointi 47 za mechi 20 ni ya tatu.
    Simba SC walimiliki zaidi mpira na kutengeneza nafasi nyingi, lakini ikawa vigumu tu kutumbukizwa mpira nyavuni, wakati Prisons waliocheza kwa kujihami zaidi hawakulifikia mara nyingi lango la wenyeji wao.
    Ushindi huo ni kisasi kwa Simba baada ya kufungwa 1-0 na Prisons katika mchezo wa kwanza wa Ligi Kuu msimu huu Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya.
    Wachezaji wa Simba wakiwa wamemzingira mfungaji wa bao lao, Awadh Juma Issa kumpongeza
     

    Mchezo mwingine wa Ligi Kuu leo, Mgambo JKT imelazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 na Mwadui FC ya SHinyanga Uwanja wa Mkwakwani, Tanga, wakati jana Mtibwa Sugar imeifunga 2-1 JKT Ruvu Uwanja wa Manungu, Turiani, Morogoro.
    Kikosi cha Simba SC kilikuwa: Vincent Angban, Hassan Kessy, Mohammed Hussein, Novaty Lufunga, Juuko Murshid, Justice Majabvi/Awadh Juma, Mwinyi Kazimoto, Jonas Mkude, Ibrahim Ajibu, Hamisi Kiiza/Paul Kiongera dk83 na Mussa Mgosi/Daniel Lyanga dk46.
    Prisons: Beno Kakolanya, Salum Kimenya, James Mwasota, Lugano Mwangama, Laurian Mpalile, Jumanne Elfadhil, Lambarti Sabiyanka, Juma Seif ‘Kijiko’/Freddy Chudu dk60, Mohamed Mkopi, Jeremiah Juma/Meshack Suleiman na Benjamin Asukile.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC SHEREHE…NI SHEREHE ZA USHINDI KUELEKEA UBINGWA, PRISONS AFA 1-0 TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top