• HABARI MPYA

    Sunday, March 20, 2016

    FUNGU LA KWANZA STARS LAPAA LEO CHAD

    Na Somoe Ng'itu, DAR ES SALAAM 
    KUNDI la kwanza la wachezaji wa timu ya soka ya Taifa (Taifa Stars) linaondoka leo kuelekea N'Djamena nchini Chad kwa ajili ya mechi ya kwanza ya kuwania tiketi ya kucheza fainali zijazo za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON).
    Mechi kati ya Chad na Taifa Stars itafanyika Jumatano Machi 23 mwaka huu na marudiano itacheza Machi 28 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
    Akizungumza na gazeti hili jana, kocha mkuu wa Taifa Stars, Boniface Mkwasa, alisema kuwa uamuzi wa kuondoka kwa 'mafungu' umetokana na baadhi ya wachezaji walioitwa kwenye timu hiyo kuwa na majukumu ya klabu nje ya Dar es Salaam.
    Kutoka kulia ni beki Kevin Yondan, kiungo Deus Kaseke na beki Mohammed Hussein 'Tshabalala'

    Mkwasa alisema kuwa wachezaji wanaocheza nje ya nchi nahodha Mbwana Samatta wa KRC Genk ya Ubelgiji na Thomas Ulimwengu wa TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) wataungana na timu hiyo huko huko N'Djamena.
    "Tumefanya hivi ili kupata nafasi angalau ya kufanya mazoezi kwa siku tatu tukiwa huko huko Chad, ratiba ya Ligi Kuu na mashindano ya kimataifa ya Klabu Bingwa Afrika na Kombe la Shirikisho imetubana makocha wa timu za taifa safari hii, tutakutana na wachezaji muda mfupi kabla ya mechi," alisema Mkwasa.
    Kocha huyo aliongeza kwamba licha ya changamoto hiyo, bado Taifa Stars ina nafasi ya kuanza vyema kampeni hizo kwa sababu alikuwa akifanya mawasiliano na wachezaji kwa ajili ya kuwaandaa na mchezo huo wa ushindani.
    Stars itafanyika Jumatano Machi 23 mwaka huu na marudiano itacheza Machi 28 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
    Wakati huo huo: Timu ya soka ya Taifa ya Wanawake, Twiga Stars inatarajiwa kuwakabili wenyeji wao Zimbabwe (Mighty Warriors) katika mchezo wa marudiano wa kusaka tiketi ya kushiriki fainali zijazo za Kombe la Mataifa ya Afrika (AWC) utakaofanyika leo kwenye Uwanja wa Rufalo jijini Harare.
    Katika mchezo wa kwanza uliofanyika Machi 4 kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi jijini Dar es Salaam, Twiga Stars ililala mabao 2-1 dhidi ya wapinzani wao hao na leo inahitaji ushindi wa kuanzia 2-0 ili iweze kusonga mbele.
    Kocha mkuu wa Twiga Stars, Nasra Juma, alisema kwamba kikosi chake kiko tayari kwa mapambano na wanataka kurudia mafanikio waliyopata 2010 kwa kushiriki fainali hizo zilizofanyika jijini Johannesburg, Afrika Kusini.
    Nasra alisema kuwa sasa wanaingia mchezo wakiwa wanawafahamu wapinzani wao tofauti na ilivyokuwa katika mechi ya kwanza ambayo walikubali kichapo.
    "Tunajua aina ya wachezaji na mfumo wanaocheza, tumejipanga kufanya vizuri kwa sababu nia, sababu na uwezo wa kuwaondoa Zimbabwe wakiwa kwao tunao," alisema Nasra.
    Mkuu wa msafara wa timu hiyo na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Amina Karuma, aliliambia gazeti hili kwa njia ya simu kwamba wachezaji wote wako katika hali nzuri na wanasubiri muda wa mchezo ufike.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: FUNGU LA KWANZA STARS LAPAA LEO CHAD Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top